Habari za Kitaifa

Rais kuhutubia Bunge la Kaunti kwa mara ya kwanza katika historia

Na KEVIN CHERUIYOT April 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

RAIS William Ruto atahutubia Bunge la Kaunti ya Nairobi hii leo, tukio ambalo ni la kihistoria kwani halijawahi kufanywa na marais wanne waliohudumu hapo awali.

Kwenye barua kwa Spika wa Bunge la Kaunti Kennedy Ngóndi, Mkuu wa Utumishi wa Umma Felix Koskei alithibitisha kuwa Rais Ruto atawahutubia madiwani Alhamisi kwa mwaliko wa bunge.

“Kutokana na barua yako ya Februari 18, 2026 iliyomwalika Rais kuhutubia Bunge la Kaunti mnamo Aprili 9, 2026, nakuarifu kuwa shughuli hiyo imeratibiwa kufanyika Alhamisi saa nane unusu katika majengo ya bunge la kaunti. Naomba uwasilishe maelezo yoyote kwa afisi hii ili yatumiwe na Rais,” akasema Bw Koskei.

Wiki jana, Gavana wa Nairobi Johnson Sakaja alisema mwaliko kwa rais unaonyesha uhusiano unaoendelea kuimarika kati ya serikali ya Kaunti na ya Kenya Kwanza.

“Tumekubali kwamba aje na azungumze na madiwani na ninafikiria ni hatua ambayo inaimarisha ugatuzi. Anastahili kufanya hivyo kwa kaunti nyingine pia,” akasema Bw Sakaja.

Rais anatarajiwa kuzungumzia uhusiano wa serikali kuu na Kaunti ya Nairobi ambayo mkataba wa Sh80 bilioni ulitiwa saini kwenye Ikulu ya Nairobi mnamo Februari.

Mkataba huo unasema kaunti itashirikiana na serikali kuu kupambana na changamoto za Kaunti ya Nairobi.
Pia kiongozi wa nchi anatarajiwa kuzungumzia suala tata la uzoaji wa taka kutokana na malalamishi kuwa jiji la Nairobi ni chafu.

Serikali kuu ishajitwalia jukumu la kusafisha Nairobi pamoja na Mto Nairobi. Pia Rais atazungumzia jiji kuunganishiwa maji pamoja na miradi ya kuimarisha miundomsingi yake inayotekelezwa sehemu mbalimbali hadi leo.

Haya yanajumuisha ahadi ya kuweka lami kwenye kilomita kadhaa barabarani na kuweka taa sehemu mbalimbali jijini.

Ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, masoko ya kisasa na kujengwa upya kwa soka la Gikomba pia ni baadhi ya masuala anayotarajia kuzungumzia.

Ziara hiyo inakuja baada ya Rais na marehemu Raila Odinga kuingilia kati mwaka jana na kuwazuia madiwani kumwondoa madarakani Gavana Sakaja.