Viwango vya utuzaji wakati wa kusahihisha Insha
SIKU ya leo tutarejelea baadhi ya viwango mbalimbali vya utuzaji wa insha kuanzia D- hadi B wasatani. Kila insha huwa na jumla ya alama 20.
D – alama 01- 02
1. Insha ya namna hii haina mpangilio maalum na haieleweki kwa vyovyote vile.
2. Insha hailandani na swali lililoulizwa.
3. Insha iliyoandikwa kwa lugha isiyo sahihi au kuchanganya ndimi.
4. Kunakili swali au maswali na kuyakariri.
5. Kunakili swali au kichwa pekee.
D (wastani) alama 03
1. Mtiririko wa mawazo haupo.
2. Mtahiniwa amepotoka kimaudhui.
3. Matumizi ya lugha ni hafifu mno.
4. Kuna makosa mengi ya kila aina.
D+ alama 04 – 05
1. Insha ina makosa mengi ya kila aina, lakini unaweza kutambua kile ambacho mtahiniwa anajaribu kuwasilisha.
2. Hoja hazikuelezwa kikamilifu au mada haikukuzwa vilivyo.
3. Mtahiniwa hana uhakika wa matumizi ya lugha.
4. Mtahiniwa hujirudiarudia.
5. Insha imezingatia sura lakini imekosa maudhui.
6. Insha ya urefu wa robo, yaani, isiyozidi maneno 174.
C- alama 06-07
1. Mtahiniwa ana shida ya kuwasilisha na kutiririsha mawazo/maudhui yake.
2. Mtahiniwa hana msamiati wa kutosha wala miundo ya sentensi ifaayo.
3. Mtahiniwa anafanya makosa mengi ya sarufi, ya hijai na ya msamiati na insha haieleweki kwa urahisi.
C alama 08
1. Mtahiniwa anawasilisha ujumbe lakini kwa njia hafifu.
2. Dhana tofauti hazijitokezi wazi.
3. Mtahiniwa hana ubunifu wa kutosha.
4. Mtahiniwa hana ufundi wa lugha unaofaa na mtiririko wa mawazo ni hafifu.
5. Mtahiniwa amejaribu kuishughulikia mada aliyopewa.
6. Mtahiniwa ana shida ya uakifishaji.
7. Mtahiniwa anafanya makosa mengi ya sarufi, ya hijai na msamiati lakini bado insha inaeleweka.
C+ alama 09-10
1. Mtahiniwa anawasilisha ujumbe vizuri akizingatia mada na hivyo insha inaeleweka.
2. Dhana tofauti zimejitokeza japo kwa njia hafifu.
3. Kuna mtiririko wa mawazo japo hana ufundi wa lugha unaofaa.
4. Misemo na methali zimetumika kwa njia hafifu.
5. Mtahiniwa ana shida ya uakifishaji.
6. Kuna makosa ya sarufi, msamiati na hijai yanayoathiri mtiririko wa mawazo.
7. Insha ya kiwango cha nusu, yaani maneno 175- 274 isizidi kiwango hiki.
B – alama 11- 12
1. Anawasilisha ujumbe vizuri kwa kueleza hoja tofauti akizingatia mada.
2. Ana mtiririko mzuri wa mawazo.
Anatumia mifano michache ya msamiati unaovutia.
3. Makosa si mengi.
B alama 13
1. Anadhihirisha hali nzuri ya kuimudu lugha.
2. Mawazo yake yanadhihirika akizingatia mada.
3. Anateua na kutumia mifano michache ya msamiati mwafaka.
4. Sarufi yake ni nzuri.
5. Makosa ni machache.