Osotsi ‘alipigwa Kisumu kwa kupinga Tutam’
SENETA wa Vihiga, Godfrey Osotsi jana alipigwa na vijana katika mkahawa mmoja Kisumu kabla ya kuokolewa na kutibiwa katika hospitali moja jijini humo.
Mkurugenzi wa Mawasiliano wa Bw Osotsi, Derick Luvega, alisema bosi wake alipigwa na kundi la vijana waliokuwa na silaha.
Seneta huyo alikuwa ametembelea duka la Jumla la Westend kunyolewa kisha akaenda mkahawa wa Java kukutana na rafiki ndipo akazungumza na umma kwa dakika 30 hivi.
Ni wakati huo ambapo kundi la vijana waliojihami walimfikia na kuzua maswali kuhusu msimamo wake wa kisiasa kabla ya kuanza kumpiga.
Vijana hao walitaka kufahamu kwa nini amekuwa akipinga kuchaguliwa tena kwa Rais William Ruto ilhali ODM ishaamua kumuunga Rais mnamo 2027.
“Walinzi wake walijizuia sana kutumia bunduki zao na wangefanya hivyo basi wananchi wangeumia,” akasema Bw Luvega.
Alitoa wito kwa Tume ya Huduma kwa Polisi (NPS) ichunguze suala hilo kwa undani kisha ichukue hatua dhidi ya wahusika.
“Kuna kanda ya CCTV Java ambayo itasaidia kuwatambua wale ambao walishiriki kitendo hiki. Sheria lazima itekelezwe na walioshiriki kitendo hiki lazima wachukuliwe hatua kali,” akaongeza Bw Luvega.
Bw Osotsi majuma mawili yaliyopita alitimuliwa kama naibu kiongozi wa ODM na siasa zake zinaegemea mrengo wa Linda Mwananchi unaoongozwa na Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna.