Junet aonya Ruto asichezee ODM shere kuhusu 2027
KATIKA kile kinachoashiria mpasuko mkubwa ndani ya Serikali Jumuishi, chama cha ODM sasa kinatishia kujiondoa katika ushirikiano huo kikidai wabunge wake wananyanyaswa na kulazimishwa kuhamia chama cha UDA kinachoongozwa na Rais William Ruto.
Chama hicho kimesema kuna matumizi ya vitisho na rasilimali za serikali katika mpango wa kukidhoofisha na kukigeuza kuwa chama cha eneo la Nyanza pekee, hasa miongoni mwa Waluo, ili kupunguza nguvu Zake katika mazungumzo ya muungano wa kabla ya uchaguzi wa 2027.
Katika mahojiano maalum, Kiongozi wa Wachache Junet Mohammed, alisema kuna njama ya makusudi inayoratibiwa na maafisa wa juu serikalini wanaohofia uwepo wa ODM katika Serikali Jumuishi.
Alisema kuingizwa kwa wanachama wa ODM serikalini hakukuwa hisani, bali zilikuwa juhudi za kuimarisha umoja na maendeleo nchini kama ilivyokusudiwa na aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga kabla ya kifo chake Oktoba mwaka jana.
“Hatuko serikalini kwa bahati au kwa mwaliko. Tuliingia kuleta umoja na ujumuishaji. Ikiwa ajenda hiyo haipo tena, waeleze wazi kwa sababu hatuna uhaba wa kimbilio,” alisema Bw Mohammed.
ODM sasa imeitisha mkutano wa dharura wa Kamati Kuu ya Usimamizi (CMC) kujadili hali ya kisiasa iliyopo, huku ikionya kuwa mvutano unaweza kuongezeka ikiwa malalamishi yao hayatashughulikiwa.
Bw Mohammed alidai kuwa wabunge wa ODM, hasa kutoka Pwani na Magharibi, wanashinikizwa kujiunga na UDA.
Aidha, alisema hata wanachama wa ODM walioteuliwa serikalini wanatishwa ili wajitenge na chama hicho.
“Watu tuliowapeleka serikalini wanaonywa wasihusiane na ODM. Hii lazima ikome.”
Sio hisani kuwa serikalini,” alisema.
Mzozo huo unajiri huku ODM ikionyesha nia ya kudai nafasi ya Naibu Rais katika mazungumzo ya muungano wa kabla ya uchaguzi, jambo ambalo limezua mvutano na wandani wa Naibu Rais Profesa Kithure Kindiki.
Kwa upande wake, Naibu Gavana wa Kakamega Ayub Savula alidai kuwa wabunge wengi wa ODM kutoka kaunti hiyo wako tayari kuhamia UDA kabla ya uchaguzi ujao, akipuuza wazo la kutengewa maeneo.
Wakati huo huo, Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo alitoa wito kwa Rais Ruto na kiongozi wa ODM Oburu Oginga kuunda timu za mazungumzo kushughulikia masuala tata kama kutenga maeneo.
“Muda unasonga. Tunapaswa kuwa tayari na mikakati mapema iwapo mazungumzo yatashindikana,” alisema.