Washirika wa Ruto ‘wanaomchomea kura’ uchaguzi wa 2027
VIONGOZI wakuu wa kisiasa na usalama ndani ya serikali ya Rais William Ruto wanakumbwa na msukosuko wa kisiasa unaotishia kuvuruga Serikali Jumuishi na kuchochea upinzani dhidi ya utawala wa Kenya Kwanza kuelekea uchaguzi wa 2027.
Baadhi ya maafisa hao wanadaiwa kujihusisha na mvutano kwa lengo la kujihakikishia mustakabali wao wa kisiasa mwaka 2027 na pia kuimarisha nafasi ya Rais Ruto, huku hatua zao zikifichua udhaifu wa ndani wa serikali hiyo.
Vurugu katika mikutano ya upinzani zinazosababishwa na polisi na makundi ya wahuni, zimechochea ukosoaji mkali, huku madai ya matumizi ya rasilimali za umma kuimarisha kampeni za Rais yakizidi kuibuka.
Ndani ya serikali hiyo, chama cha Orange Democratic Movement (ODM) kimewashutumu baadhi ya maafisa wakuu kwa madai ya kuwahonga wabunge wake kwa mamilioni ya pesa ili wahame chama hicho na kujiunga na United Democratic Alliance (UDA).
Inadaiwa wabunge hao wanaahidiwa fedha za kampeni ili kudhoofisha nguvu ya ODM katika mazungumzo ya miungano kabla ya uchaguzi.
Naibu Rais Kithure Kindiki, Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen, Katibu wa Wizara hiyo Raymond Omollo na Kiongozi wa Wengi Bungeni Kimani Ichung’wah wamekuwa wakilaumiwa na wanasiasa wa upinzani na hata wale wanaounga mkono serikali.
Katika eneo la Mlima Kenya, aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua amemlaumu Ichung’wah kwa vurugu zilizoshuhudiwa Kikuyu, huku Ichung’wah naye akimlaumu Gachagua kwa hali hiyo.
Murkomen na Omollo pia wamekabiliwa na shutuma kutokana na ongezeko la mashambulizi ya makundi ya wahuni, hasa baada ya kushambuliwa kwa Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi.
Mvutano ndani ya serikali uliwekwa wazi na Kiongozi wa Wachache Bungeni Junet Mohammed aliyedai kuwa kuna njama ya kuwahonga wabunge wa ODM.
“Wabunge wetu wanapewa pesa wajiunge na UDA. Huu ni mpango wa kuifanya ODM kuwa ya eneo la Luo Nyanza pekee,” alisema.
Chama hicho kimetishia kujiondoa serikalini iwapo Rais hataingilia kati.
Hata hivyo, viongozi wa UDA wamekanusha madai hayo. Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa alisema wanaojiunga na chama hicho wanafanya hivyo kwa hiari kutokana na umaarufu wake.
Naye Naibu Gavana wa Kakamega Ayub Savula alikanusha madai ya hongo, akisema alihama kwa hiari yake.
Katika eneo la Nyanza, Omollo amekuwa katika mvutano wa kisiasa huku baadhi ya wanasiasa wakimlaumu kwa kuimarisha UDA huku akidhoofisha ODM.
Wabunge kadhaa akiwemo Millie Odhiambo na Jared Okello walimtetea, wakisema hana makosa.
Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino wanataka achunguzwe na hata kukamatwa kufuatia madai ya kuhusika na vurugu.
Dkt Omollo amekanusha madai hayo akisema serikali haitavumilia uhalifu na vurugu za kisiasa.
Murkomen naye aliwataka viongozi kujitenga na siasa za vurugu na kuhimiza mjadala wa sera badala ya fujo.
Hata hivyo, Naibu Kiongozi wa chama cha Jubilee Jeremiah Kioni alisema kuna mwelekeo wa mikutano ya upinzani pekee kushambuliwa, jambo linalozua maswali kuhusu ushiriki wa serikali.
Gachagua naye alisisitiza kuwa vitisho na matumizi ya nguvu havitaweza kuzuia mabadiliko ya kisiasa.
Mvutano huu unaibuka wakati hali ya kisiasa nchini in inazidi kuwa tete, huku kila upande ukijipanga kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.