Siasa

Jiandae kwa mwaka mgumu, Kalonzo amuonya Ruto

Na ANTHONY KITIMO August 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KIONGOZI wa Wiper Patriotic Party, Kalonzo Musyoka, amemuonya Rais William Ruto kwamba mwaka wake wa mwisho mamlakani utakuwa mgumu, huku upinzani ukiahidi kuongeza ukosoaji wa serikali kuelekea uchaguzi wa 2027.

Bw Musyoka alisema sauti ya upinzani itabadilika na kuwa kali zaidi katika siku 365 zijazo, huku akimshutumu Rais Ruto kwa kukiuka Katiba na kushindwa kutekeleza ahadi za manifesto ya Kenya Kwanza.

“Tutaweka kila kitu wazi na kuwaeleza Wakenya jinsi Rais Ruto amekiuka Katiba na kufanya kinyume na manifesto yake,” alisema.

Kiongozi huyo wa Wiper alianza ziara ya siku tano Pwani Jumatano, akitarajiwa kuzuru Kwale, Kilifi, Mombasa na Taita-Taveta.

Alianza ziara hiyo kwa kuhudhuria mkutano mkuu wa kila mwaka wa Chama cha Wanasheria nchini (LSK) huko Diani, Kwale, kabla ya mikutano ya kisiasa katika maeneo mbalimbali ya Pwani.

Bw Musyoka pia alitumia ziara hiyo kushinikiza serikali kutatua mzozo wa kidiplomasia kati ya Kenya na Sudan uliosababisha kusimamishwa kwa uuzaji wa bidhaa za Kenya, ikiwemo chai.

Sudan ilisimamisha uagizaji wa bidhaa kutoka Kenya Machi 2025 baada ya Nairobi kuandaa mkutano wa viongozi wa wanamgambo wa Rapid Support Forces (RSF), hatua ambayo Khartoum ilisema ilikuwa kuingilia masuala yake ya ndani.

Kabla ya marufuku hiyo, Sudan ilikuwa ikiagiza takriban kilo milioni 35 za chai ya Kenya kila mwaka, zenye thamani ya dola milioni 69.

Bw Musyoka alisema amekutana na Balozi wa Sudan nchini Kenya, Kamal Gubara, na kujadili namna ya kumshawishi Rais wa Sudan, Jenerali Abdel Fattah al-Burhan, kuondoa marufuku hiyo.

“Tulipatana kwamba atapeleka mazungumzo kwa viongozi wa juu ili kuomba Rais Burhan aondoe marufuku na kuwezesha biashara kati ya Kenya na Sudan,” alisema.

Bw Musyoka pia aliishutumu serikali kwa madai ya kuruhusu bandari ya Mombasa kutumiwa kuingiza silaha zinazolengwa Sudan, akisema hatua hiyo imechangia kuzorota kwa uhusiano kati ya nchi hizo mbili.

Wakati huo huo, Mkurugenzi Mkuu wa East Africa Tea Trade Association George Omuga, alisema zaidi ya kilo milioni 3.44 za chai zenye thamani ya zaidi ya dola milioni 10.3 bado zimekwama katika maghala ya Mombasa.

Alisema chai hiyo ilikuwa imechanganywa na kufungashwa maalum kwa ajili ya soko la Sudan na hivyo ni vigumu kuipeleka katika masoko mengine.

Bw Omuga alisema kufunguliwa kwa soko la Sudan kutawasaidia wakulima, wafanyabiashara na wauzaji wa chai nchini Kenya.