Habari za Kitaifa

Wandayi: Nitajiuzulu vipi na mafuta yapo tele, na pia sijahusika kwenye kashfa

Na DAVID MWERE April 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WAZIRI wa Kawi na Petroli, Bw Opiyo Wandayi, amefichua kuwa aliachwa gizani kuhusu mpango wa kuingizwa nchini kwa mafuta ya thamani ya Sh12 bilioni katika sakata inayoendelea, akisisitiza kuwa shughuli hiyo ilifanyika nje ya mfumo wa Serikali kwa Serikali (G-to-G).

Bw Wandayi aliambia Kamati ya Bunge kuhusu Kawi, inayoongozwa na Mbunge wa Nakuru Town East, David Gikaria, kwamba kama angehusishwa mapema, angepeleka suala hilo kwa Baraza la Mawaziri kupata idhini rasmi.

Alisema kuwa baada ya kugundua kuhusu uingizaji huo, alimwagiza aliyekuwa Katibu wa Petroli, Mohamed Liban, ambaye amejiuzulu, kuchukua hatua za kuhakikisha kampuni husika inafuata mwongozo wa serikali.

Hatua hizo zilijumuisha kuagiza kampuni ya One Petroleum, iliyoingiza mafuta hayo, kuyaondoa nchini na kufuta vocha zote za madai ya malipo zilizotolewa kwa wauzaji wa mafuta nchini.

“Idhini ya Waziri katika uingizaji wa mafuta haya haikutafutwa,” alisema Wandayi, akiongeza kuwa “hakuna sababu ya kumfanya asiendelee kutekeleza majukumu yake kama Waziri”.

Alikuwa akijibu maswali ya wabunge waliotaka kujua kuhusika kwake katika mkataba huo.

“Lau jambo hili lingefikishwa kwangu, ningelipeleka juu zaidi, kwa Rais na Baraza la Mawaziri kwa hatua zinazofaa,” alisema.

Bw Wandayi alisema kuwa mfumo wa G-to-G ni mpango unaotokana na maamuzi ya Baraza la Mawaziri na unaongozwa na sheria, hivyo basi mabadiliko yoyote yanahitaji idhini ya baraza hilo.

Bw Liban, Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya Kenya Pipeline (KPC) Joe Sang, na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Kawi na Petroli (EPRA) Daniel Kiptoo walijiuzulu kutokana na sakata hiyo iliyoibuka wakati wa likizo ya Pasaka.

Liban anadaiwa kuhalalisha uingizaji wa mafuta hayo akisema ulilenga kukabiliana na upungufu wa hifadhi ya mafuta nchini kutokana na vita vya Mashariki ya Kati, kati ya Amerika-Israel na Iran.

Hata hivyo, waziri huyo alidokeza uwezekano wa kuwepo kwa upotoshaji wa takwimu za akiba ya mafuta ili kuhalalisha uagizaji huo.

Ingawa maafisa hao walidaiwa kuzuiliwa na polisi kwa wikendi ya Pasaka, bado hawajafikishwa mahakamani huku Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) ikiendelea na uchunguzi.

Bw Wandayi alieleza kamati ya bunge kuwa hawezi kufahamu sababu halisi ya kujiuzulu kwao, akikanusha madai kwamba walilazimishwa kuondoka ofisini.

“Sijui kwa nini walijiuzulu,” alisema, akiongeza kuwa kujiuzulu ni uamuzi wa mtu binafsi.

Alipoulizwa kuhusu uwezekano wa kupanda kwa bei ya mafuta katika marekebisho ya kila mwezi yanayotarajiwa kutangazwa na EPRA leo, Wandayi alisema hawezi kutabiri hali itakavyokuwa.

“Sijui EPRA watatangaza nini. Lakini hatujatulia. Tunachukua hatua za mapema, ikiwemo masuala ya ushuru, kuhakikisha wananchi hawathiriwi na hali ilivyo Mashariki ya Kati,” alisema.

Mzozo kuhusu Mkondo wa Hormuz umeathiri usafirishaji wa mafuta duniani baada ya meli kupungua kwa kiasi baada ya mlango-bahari huo kufungwa na Iran.

Mkondo huo ni njia pekee ya baharini kutoka Ghuba ya Uajemi (Iran) kuelekea Bahari ya Oman na Bahari ya Arabia, na ni njia muhimu zaidi ya usafirishaji wa mafuta duniani.

Takribani asilimia 20 hadi 25 ya mafuta yanayosafirishwa baharini duniani hupitia eneo hilo, pamoja na asilimia 20 ya gesi asilia (LNG).

Waziri Wandayi alikiri kuwa hali ya sasa imechangia kupanda kwa bei ya mafuta duniani, lakini akasema EPRA itatoa taarifa rasmi kuhusu hatua za kuwalinda wananchi dhidi ya gharama hizo.