Lugha, Fasihi na Elimu

Hivi ni sahihi kutumia neno ‘nyanja’ kwa maana ya umoja na wingi?

Na IRIBE MWANGI August 5th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JUMA hili nimesisimshwa na Makala yaliyoandikwa na mweledi mashuhuri wa lugha ya Kiswahili Ustadh Abdilatif Abdalla.

Japo yeye daima hunyenyekea kwamba si msomi wa Kiswahili, mimi humuona kama mmoja kati ya wabobezi wachache wa Kiswahili, Uswahili na fasihi yake.

Daima mimi huchukizwa na matumizi ya *nyimbo hii (na ninafikiri niliona Prof. F. E. M. K. Senkoro pia akitaja hilo) na kwa sababu hiyo maelezo ya Ustadh yalinichangamsha mno!

Kwa kuwa Ustadh aliyaandika maelezo yake katika kumbi za umma kwa kusudi la kuelimisha, naomba niyanukuu neno kwa neno.

“… neno nyanja ni wingi wa uwanja. Kwa hivyo, kwa maoni yangu mimi mzungumzaji wa Kiswahili wa kawaida tu (ambaye si mtaalamu wala si msomi), si sawa, wala si Kiswahili fasaha, wala si Kiswahili Sanifu, kulitumia neno nyanja kama kwamba umoja wake na wingi wake ni huo huo.

Kuna na maneno mengine (ambayo nitayaorodhesha hapa chini) yaliyotiwa katika mkumbo huo wa matumizi ya makosa, kama hilo nyanja, kiasi cha kwamba wale wasioujua usuli wa maneno hayo haiwapitikii kamwe kuwa wafanyayo ni makosa!

Na baadhi yayo yamekuwa yakitumiwa kwa makosa kwa muda mrefu (hata na wale wanaoshughulika na kukisanifu Kiswahili!) mpaka leo imekuwa ukimtanabahisha mtu kuwa hayo ni makosa, wewe mtanabahishaji ndiye utakayeonekana kuwa unakosea.

Nimewahi kuambiwa na baadhi ya wataalamu wetu wa Sarufi na Isimu kwamba makosa yafanyikayo katika/kwenye lugha, na yakazowewa na baadhi ya watu na yakaendelea kufanywa kwa muda mrefu, makosa hayo huweza kukubaliwa kuwa sahihi.

Kama nilivyotangulia kueleza, mimi si mtaalamu wala si msomi wa lolote. Kwa hivyo, napata tabu kuikubali hoja (huja) hii.

Mtaniwia radhi wataalamu na wasomi. Huenda nisingekuwa na shida hiyo kama nami ningekuwa nimejaaliwa kuwamo katika/kwenye matengo hayo.

Na linipalo tabu zaidi ni kuona jinsi baadhi yetu tulivyojipa leseni ya kuyafanya makosa kama haya kwa wepesi mno na (pengine) bila kujali, na kwa sababu hiyo niliyoieleza.

Lakini huwa twalifanya hilo humu Kiswahilini tu. Hatuthubutu kulifanya hilo kwenye lugha za kigeni tujifunzazo.

Huko huwa tuna hadhari sana, na hufanya juhudi kubwa, tusionekane tumefanya makosa.

Na mtu huwa haachiliwi kuendelea kuyafanya makosa, hata kama makosa hayo yamekuwa yakitumiwa na baadhi ya watu kwa muda mrefu.

Kwa nini, basi, makosa kama hayo yawe yanakubalika katika/kwenye hiki tukiitacho Kiswahili Sanifu? Naelewa, na ninakubali, kwamba nje ya Kiswahili fasaha na sanifu watu watakitumia Kiswahili vile watakavyo wao wenyewe, maadamu watakuwa wanaelewana wenyewe kwa wenyewe.

Lakini tushughulikapo na Kiswahili fasaha na sanifu, yatubidi tuweke mipaka. Tusikifanye Kiswahili kama kwamba ni ng’ombe asiyekuwa na mchunga.

Haya yafuatayo ni baadhi tu ya maneno ambayo wengine wetu tumekuwa tukitumia wingi wake kuwa ni umoja.

Maneno yaliyoko kushoto yamo katika hali ya umoja, na yaliyo kulia ni wingi wayo:

Wenzo (huu) – nyenzo (hizi)

Usimulizi (huu) – simulizi (hizi)

Utanzu (huu) – tanzu (hizi)

Utungo (huu) – tungo (hizi)

Ubeti (huu) – beti (hizi)

Uga (huu) – nyuga (hizi)

Uchango (huu) – chango (hizi)

Waraka (huu) – nyaraka (hizi)

Utumbuizo (huu) – tumbuizo (hizi)

Wimbo (huu) – nyimbo (hizi)

Juma lijalo nitaendeleza makala haya kwa kutoa hoja zilizotolewa na Prof Kineene wa Mutiso wakati akitoa jibu kuhusu makala haya.