Habari za Kitaifa

Ruto: Hakuna mtu yeyote saizi yangu huko Upinzani; na kwanza hawanijui vizuri

Na RUTH MBULA April 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

RAIS William Ruto amewashutumu wapinzani wake wa kisiasa kwa kile alichokitaja kuwa kutumia vitisho na kauli zisizo na mashiko, akionya kuwa mbinu hizo hazitafanikiwa kumwondoa madarakani.

Akizungumza kwa ukali dhidi ya viongozi walioko chini ya mwavuli wa Muungano wa Serikali Mbadala (Upinzani), Dkt Ruto alisisitiza azma yake ya kuwalinda wananchi dhidi ya vitisho vya kisiasa, akiahidi kuendeleza misingi ya demokrasia na ushirikishaji.

Akizungumza akiwa katika Kaunti ya Nyamira wakati wa ziara ya maendeleo, Rais alisema hataruhusu upinzani kuharibu nchi kwa jina la siasa.

“Nchi hii ni ya wananchi wote wala hakuna mtu atakayewatisha wengine. Hawawezi kutuambia kwamba wataondoa rais. Kenya si ya watu wachache bali ya Wakenya wote,” alisema.

Aliongeza kuwa ni Wakenya pekee ndio wanaoweza kuamua mustakabali wa taifa, akionyesha imani kuwa hakuna kiongozi wa upinzani aliye na uwezo wa kumshinda katika uchaguzi mkuu wa 2027.

“Je, wananijua kweli? Hakuna aliye na uzito wa kisiasa, maono na rekodi ya kunishinda. Waache kiburi na chuki. Wanasema wanaweza kutishia Jamhuri ya Kenya, kuondoa viongozi na nchi kusimama. Kenya haitafeli; ni wao watakaoshindwa,” alisema Rais.

Alisisitiza kuwa wapinzani hawawezi kumtisha, akisema hawamfahamu vizuri.

Rais Ruto aliandamana na Naibu wake Profesa Kithure Kindiki pamoja na viongozi kadhaa wa eneo la Gusii wakiongozwa na Gavana wa Nyamira Amos Nyaribo.

Mnamo Jumapili, Rais alikutana na viongozi waliochaguliwa wa Gusii katika Ikulu Ndogo ya Kisii katika mkakati wa kuimarisha uungwaji mkono wake katika eneo hilo.

Katika mkakati huo, alialika zaidi ya madiwani 70 kutoka Kisii na Nyamira aliowahimiza kumuunga mkono kupata muhula wa pili.