Majuto ya ajuza aliyetekwa na uraibu wa Aviator — hutumia pesa za matibabu kuweka beti
SIMULIZI ya familia moja kutoka mtaa wa Pipeline imefichua kwa kina madhara ya uraibu wa kamari unaozidi kushika kasi nchini.
Binti mmoja aliyetambulika kama LM aliwasilisha malalamiko makali kuhusu mamake, WA, ambaye licha ya kuugua saratani, hawezi kuacha kamari.
LM alisema amechoshwa na tabia hiyo, hasa baada ya kugundua kuwa mama yake hutumia pesa muhimu kwa mahitaji ya familia kuweka beti.
Katika mahojiano, LM alisimulia tukio lililomvunja moyo alipomtumia mamake pesa ili aandalie mtoto wake chakula cha mchana.
Aliporejea nyumbani jioni, hakukuwa na chakula -pesa zote zilikuwa zimeishia kwa kamari.
LM alisema alianza kufuatilia M-Pesa ya mamake na kugundua alikuwa akipoteza pesa nyingi kwa kampuni za kamari.
Aliongeza kuwa mamake sasa anakopa pesa ili kuendeleza uraibu huo.
“Nakupenda kama mama yangu, lakini sasa nimeamua kukupenda nikiwa mbali. Nataka amani tu,” alisema LM.
Mama huyo, WA, alikiri kuwa na uraibu wa kamari lakini akaomba kutotajwa jina lake kwa sababu anategemea msaada wa kifedha kutoka kwa watu wengine kupambana na ugonjwa wake.
Alisema alianza kubeti mwaka wa 2017, baada ya kutembelea vibanda vya kamari na kuvutiwa na watu waliokuwa wakijadili bahati nasibu.
Kwa kuwa hakuwa na simu ya kisasa wakati huo, alitumia mfumo wa SMS na USSD kuweka beti (dau).
“Niliingia nikiwa na matumaini ya kuwa tajiri siku moja, lakini hilo halijawahi kutimia,” alisema.
Alikumbuka siku moja aliposhinda Sh16,000 baada ya kubashiri matokeo ya michezo kadhaa, jambo lililompa hamasa ya kuendelea.
Hata hivyo, ushindi huo mdogo ulimzidishia tamaa badala ya kumsaidia kujiondoa.
Baadaye alihamia mchezo wa Aviator, ambao humpa mchezaji nafasi ya kushinda au kupoteza pesa ndani ya sekunde chache.
WA alisema tangu aanze kucheza mchezo huo, aliachana kabisa na kamari za michezo.
“Nilianza kuamini nitapata pesa nyingi haraka, hasa kwa sababu ya gharama za matibabu,” alisema.
Hata hivyo, badala ya kufaidika, anasema amekuwa akipoteza pesa zote. Anaeleza kuwa mara nyingi hushinda kiasi kidogo kisha kuendelea kubeti kwa matumaini ya kupata zaidi, lakini huishia kupoteza kila kitu.
Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), uraibu wa kamari unaweza kusababisha matatizo ya afya ya akili, umaskini na hata mawazo ya kujiua.
Shirika hilo linaeleza kuwa dalili zake ni pamoja na kushindwa kudhibiti tabia ya kubeti, kuipa kamari kipaumbele kuliko mahitaji mengine, na kuendelea kubeti licha ya madhara.
WA anakiri kuwa amejaribu mara kadhaa kuacha kamari bila mafanikio. Hata hivyo, alisema hivi karibuni alifunga akaunti yake kuu ya kamari kwa siku 180, akitumai kuwa hatua hiyo itamsaidia kuacha kabisa.
“Nimechoka na hasara. Natumai sitarudi tena,” alisema.
Lakini binti yake ana mashaka, akisema hii si mara ya kwanza kwa mamake kutoa ahadi kama hiyo.
Kisa hiki kinaonyesha kwa uwazi jinsi kamari, hasa michezo ya haraka kama Aviator, inavyoathiri familia nyingi kimyakimya.
Licha ya matumaini ya utajiri wa haraka, wengi huishia katika madeni, msongo wa mawazo na migogoro ya kifamilia.
Kwa ushauri wake, WA anasema: “Afadhali ununue chakula na ujitunze kuliko kuweka pesa kwenye kamari. Mwisho wake ni majuto.”