Habari za Kaunti

Mungatana sasa apendekeza upigaji kura uwe wa lazima

Na WINNIE ATIENO April 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

SENETA wa Tana River Bw Danson Mungatana amependekeza kuwa Wakenya wote wenye vitambulisho washurutishwe kupiga kura ili wajihusishe na uchaguzi mkuu.

Hii ni baada ya kugundua kuwa zaidi ya asilimia 50 ya wakazi wa kaunti yake ambao wana vitambulisho, hawajajisajili kuwa wapigakura.

Alisema hayo kwenye zoezi la uhamasisho wa watu kujiandikisha kuwa wapigakura lililoandaliwa na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka, huko Hola Kaunti ya Tana River.

“Nimebaini kuwa wapiga kura wengi waliosajiliwa katika Kaunti ya Tana River hawajitokezi kupiga kura wakati wa uchaguzi mkuu. Nimewahimiza wakazi wa Tana River kuchukua hatua ya pili baada ya usajili wajitokeze kupiga kura wakati wa uchaguzi,” alisema Bw Mungatana.

Bw Mungatana alitoa mfano wa nchi kama Australia na Ubelgiji ambapo ni lazima mtu apige kura au alipe faini.

Barani Afrika, Misri na Gabon pia zina mfumo wa kupiga kura wa lazima.

“Matokeo yake, nchini Australia idadi ya wapiga kura wanaojitokeza hufikia asilimia 95. Ni wakati wa kuzingatia mfumo huo. Kwa hivyo ipo haja yetu kutunga sheria ya kulazimisha kupiga kura kujitokeza kwenye zoezi la uchaguzi mkuu,” alisema Bw Mungatana.

Naibu mwenyekiti wa tume ya IEBC, Bi Fahima Arafat, aliwasihi wakazi kujitokeza kujiandikisha kama wapiga kura akionya dhidi ya kuingiza siasa kwenye zoezi hilo.

Alisema ni wajibu wa Wakenya kujisajili na baadaye kujitokeza kupiga kura.