Riggy G, Kindiki wapondana kuhusu uchaguzi mdogo
ALIYEKUWA Naibu Rais Rigathi Gachagua ameongeza makali ya siasa kwa kumshambulia Naibu Rais Kithure Kindiki, akimtaja kama kiongozi asiye na msimamo na anayefuata kila agizo la Rais William Ruto bila kupinga.
Akizungumza katika mkutano mkubwa wa hadhara uliofanyika Kangema, kaunti ya Murang’a Gachagua alidai kuwa Kindiki hana ujasiri wa kushikilia misimamo yake, akimtaja kama “yes man” anayekubali kila kitu anachoambiwa na Rais.
Gachagua alidai kuwa ziara ya Kindiki huko Embu haikuvutia umma, akisema wakazi walimshangaa badala ya kumsikiliza kwa makini.
Kauli hii zinaashiria kuendelea kwa vita vya maneno kati ya viongozi hao wawili, hali inayozidi kuonyesha mpasuko wa kisiasa katika uongozi wa juu.
“Ati sasa huyu Saprano ati ndio kasongo ati ametuma mlimani ati kushindana na Riggy G. Sasa alienda Embu juzi watu wanamwangalia wanacheka. Akiamka kuongea ati kusaidia kasongo. Kwanza ni mtu ya Yes Sir. Akiambiwa kila kitu na Ruto anasema yes sir,” Gachagua alisema.
Mashambulizi haya yanajiri siku chache baada ya Gachagua kumkosoa Kindiki kuhusu siasa za uchaguzi mdogo wa Ol Kalou katika kaunti ya Nyandarua . Alimtaka kusitisha mijadala ya kisiasa hadi mbunge wa eneo hilo, marehemu David Njunguna Kiaraho, azikwe.
Gachagua alisisitiza kuwa kwa mujibu wa mila za jamii ya Wakikuyu, ni kukosa heshima kujadili mrithi wa kiongozi kabla ya mazishi kufanyika. “Hatuwezi kuzungumzia uchaguzi mdogo kabla marehemu azikwe. Hiyo ni kinyume na desturi zetu,” alisema.