Habari

ODM yakaliwa ngumu na UDA

Na BENSON MATHEKA April 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MJADALA unaoendelea ndani ya chama cha Orange Democratic Movement (ODM) wa kuhifadhiwa maeneo ya kisiasa amabyo inadai ni ngome yake, unaonyesha kimefifia na huenda kikakosa makali kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Katibu Mkuu Edwin Sifuna ameibua wasiwasi kuhusu mjadala huo akionya kuwa chama hicho kiko hatarini kupoteza ushawishi wake katika ngome zake za jadi.

Kulingana na seneta huyo wa Nairobi, ni wazi ODM imepoteza umaarufu wake kwa kiwango kinachotia shaka huku vyama pinzani kama United Democratic Alliance (UDA) vikizidi kupenya katika maeneo ambayo awali yalikuwa ngome imara ya chungwa.

Akitaja kaunti kama Homa Bay, ambayo kwa miaka mingi imekuwa ngome ya ODM, Sifuna alisema haijawahi kuhitaji mjadala kama huo.

“Kwa mara ya kwanza nasikia wito wa kuhifadhi Homa Bay. Wakati ODM ilikuwa imara hatukujali nani aligombea dhidi yetu,” alisema.

Hali ya sasa, kulingana naye, inaonyesha udhaifu unaozidi kujitokeza chamani.

Sifuna alikosoa viongozi wa chama hicho ambao wameonyesha hadharani kumuunga mkono Rais William Ruto katika azma yake ya kuwania tena 2027, akisema aliwahi kuwaonya lakini hawakumsikiliza.

Kulingana naye matokeo ya maamuzi hayo sasa yanaanza kuonekana wazi.

Kauli zake zinajiri wakati ambapo mjadala huo wa “zoning” unazidi kushika kasi ndani ya ODM, huku ukiwa mojawapo ya masharti muhimu kwenye gumzo linalotarajiwa kati ya ODM na UDA kabla kampeni za uchaguzi mkuu wa 2027 kushika kasi.

Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga amejitokeza kwa msimamo mkali akisisitiza kuwa atalinda ODM katika eneo la Nyanza.

Akizungumza katika mkutano wa hadhara Homa Bay wiki hii, Wanga, ambaye pia ni mwenyekiti wa kitaifa wa ODM, alisema chama hicho lazima kilindwe kwa vyovyote ili kudumisha nguvu zake bungeni.

“Tutalinda chama chetu. Ndilo jambo la kwanza kabla ya kitu kingine chochote,” alisema na kusisitiza kuwa mshikamano wa chama ndio msingi wa mafanikio ya kisiasa.

Viongozi wa ODM wameunga kauli hiyo wakisema ili kumuunga mkono Ruto UDA haipaswi kusimamisha wagombea katika maeneo ambayo tayari yanashikiliwa na chungwa.

Mnamo Alhamisi, Kamati Kuu Simamizi (NEC) ya ODM iliamua kusitisha kwa muda mazungumzo ya ushirikiano na UDA pamoja na kupigia debe Ruto kwa muhula wa pili, huku viongozi wakilalamika kuwa washirika wao katika Serikali Jumuishi wanawadharau.

“Kamati Kuu imebaini kwa wasiwasi mkubwa mienendo na matamshi yasiyofaa yanayotolewa na baadhi ya maafisa wa UDA yanayolenga kuleta taharuki na mgawanyiko ndani ya chama chetu,” ilisema taarifa ya chama hicho iliyosomwa na kaimu Katibu Mkuu Catherine Omanyo.

“Tunataka UDA iheshimu chama chetu, itikadi zetu na misingi ambayo tumesimika kwa muda mrefu,” alisisitiza.

Kulingana na mchanganuzi wa siasa James Owino, ODM imechelewa kuchukua hatua kwa kuwa Ruto tayari ameikata kucha.

“ Ukweli ni kwamba ujanja wa Ruto kisiasa umezima makali ya ODM. Ameifanya kuwa simba asiye na kucha za kukwaruza,” asema akirejelea mipasuko ya ndani ya chama hicho cha chungwa na hatua ya chama cha UDA kupenya ngome zake.