Habari

IEBC yapendekeza mabadiliko kadhaa ya kisheria uchaguzi wa 2027 ukikaribia

Na SAMWEL OWINO April 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka Nchini (IEBC) sasa inapendekeza mabadiliko chungu nzima ya kisheria ambazo wanataka yapitishwe kabla ya Septemba kuimarisha maandalizi na uwazi katika uchaguzi mkuu ujao.
Kati ya mapendekezo ya IEBC ni kuwa diwani maalum kwenye Bunge la Kaunti lazima awe mpiga kura katika kaunti husika, pendekezo ambalo litapigwa na wawakilishi wadi wengi kwa kuwa linawatoa tonge mdomoni.
Pia IEBC inataka majina ya jinsia ya kike yawe ya kwanza kwenye orodha ya wanaoteuliwa katika Bunge la Kitaifa, Seneti na Bunge la Kaunti kwenye kila chama cha kisiasa.
Kwa sasa majina huwa yanabadilishwa kijinsia lakini hakuna sheria yeyote inayotaka jinsi ya kike itangulie au ile ya kiume.
Aidha IEBC inataka mamlaka ya kushughulikia kesi za uchaguzi ili ziamuliwe haraka kinyume na sasa ambazo kesi hiyo huamuliwa ndani ya miezi sita lakini mchakato wa kisheria hadi mahakama ya juu huchukua kipindi kirefu.
Haya ni mapendekezo ambayo IEBC imewasilisha kwa wabunge na inataka yapitishwe kufikia Agosti 31 mwaka mmoja kabla uchaguzi wa Agosti 10, 2027.
“Kando na sheria nyingine za uchaguzi, hizi pia zinahitaji kupitishwa kabla au mnamo Septemba 2026 ili kuhakikisha IEBC inazifanyia mazoezi na mahamasisho kwa wafanyakazi wake na wapigakura,” ikasema stakabadhi ya IEBC iliyowasilishwa kwa Kamati ya Haki na Masuala ya Sheria Bunge la Kitaifa wakati wa kongamano lake hivi majuzi Mombasa.
Mapendekezo hayo yaliyoonekana na Taifa Jumapili yanahusu masuala mbalimbali, yakiwemo utambuzi wa wapiga kura, mamlaka ya uendesha mashtaka, uwasilishaji wa matokeo ya uchaguzi kutoka vituo vya kupigia kura, pamoja na uteuzi wa wabunge wa Bunge la Kitaifa, Seneti na madiwani kwenye Mabunge ya Kaunti.
Tume hiyo, katika mapendekezo yake kwa kamati inayoongozwa na Mbunge wa Tharaka George Murugara, IEBC inapendekeza Bunge kufuta Kifungu cha 20 kinachohusu ukiukaji wa Kanuni za Maadili ya Uchaguzi ili kuipatia mamlaka ya kuendesha mashtaka kuhusu makosa yanayohusiana na uchaguzi.
Tume inaeleza kuwa Mahakama ya Juu ilithibitisha kuwa jukumu hilo liko chini IEBC na Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP).
“IEBC inaomba irejeshewe mamlaka ya kushughulikia kesi na makosa ya uchaguzi kwa sababu ODPP imekuwa ikifanya wajibu wake japo kwa kujikokota,” ikasema pendekezo hilo.
IEBC pia inapendekeza kuwa mtu anayeteuliwa kwenye Bunge la Kaunti kupitia chama cha kisiasa lazima awe amesajiliwa katika gatuzi hilo.
Hii ina maana kuwa iwapo mwanasiasa amesajiliwa kama mpigakura Kaunti ya Nairobi, hawezi kuteuliwa kama diwani maalum kwenye Kaunti ya Kwale.
IEBC pia inasema sheria hiyo inastahili kutekelezwa kwa wanaoteuliwa kama seneta au mbunge maalum.
Hii ina maana kuwa iwapo mbunge au seneta maalum anateuliwa basi lazima awe amesajiliwa kutoka kaunti yake kama mpigakura.
Kwa mujibu wa sheria, vyama vya kisiasa huwa vinawasilisha majina ya watu 12 kuteuliwa kwenye Seneti au Bunge la Kitaifa.
Sheria inasema zaidi ya watu wawili kwenye orodha hiyo hawafai kutoka kaunti moja.
IEBC inataka jinsia ya kike ipewe kipaumbele kwenye orodha ya uteuzi ya vyama vya kisiasa.
Kwa sasa orodha hiyo huandaliwa bila kuweka wazi ni jinsia gani inakuja ya kwanza au ya pili.
Hii ina maana kuwa iwapo chama cha kisiasa kina nafasi moja pekee ya kumteua mtu kuwa diwani maalum, mbunge maalum au seneta maalum basi mtu huyo lazima awe mwanamke.Iwapo nafasi hizo ni tatu, basi angalau mbili zitawaendea wanawake.
IEBC inasema hatua hii itasaidia katika kuhakikisha kuna usawa wa jinsia kwenye maeneo hayo ya uwakilishi.
Pia hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa idadi ya wanawake wanaohudumu kwenye vyeo vya uwakilishi inaongezeka.
Tume hiyo pia inapendekeza kufanyiwa marekebisho kwa Kifungu cha 38A kuhusu idadi ya wapiga kura kwa kila kituo cha kupigia kura, ikitaka iongezwe kutoka 700 hadi 800.
Tume inakadiria kuwa iwapo pendekezo hilo litapitishwa na wabunge, upigaji kura katika vituo vingi utakamilika ifikapo saa 12 jioni, na hivyo kuondoa misururu mirefu ya wapiga kura kuelekea muda wa mwisho wa saa 12 jioni.
Hata hivyo, tume imeitaka kamati hiyo kuondoa kiwango cha chini cha wapiga kura 50 kwa kila kituo, ili kuzingatia maeneo ya mbali yenye mahitaji tofauti.