Hizi ndio ngome za ‘kanywaji’ – Kisii, Nairobi na Kakamega
KAUNTI za Kisii, Nairobi na Kakamega ndizo zinaongoza orodha ya kaunti ambako kiwango cha juu cha pombe haramu kimenaswa.
Hii ni kulingana na uchambuzi maalumu uliofanywa na Taifa Jumapili kutokana na ripoti iliyotolewa na Wizara ya Usalama wa Ndani kuhusu biashara ya mauzo ya pombe haramu.
Takwimu zinaonyesha kuwa Kisii inaongoza baada ya lita 353,178, kunaswa hali inayoashiria jinsi utengenezaji wa pombe za kienyeji ulivyokita mzizi katika eneo hilo.
Nairobi inafuata kwa lita 309,408, ikichochewa zaidi na kusambaa kwa pombe bandia katika soko la mijini ambako mahitaji ya bidhaa za bei nafuu ni makubwa.
Kaunti za Kakamega, Nakuru na Pokot Magharibi pia zina viwango vya juu, huku Meru, Busia, Migori, Trans Nzoia na Nandi zikikamilisha orodha ya maeneo yaliyoathirika zaidi.
Uchanganuzi wa ripoti hiyo unaonyesha jinsi ambavyo matumizi ya pombe haramu yameshika kasi Magharibi mwa nchi.
Pia unaonyesha jinsi pombe hiyo husafirishwa na kufikia miji mbalimbali bila mitego inayowekwa na maafisa wa usalama kuinasa.
Takwimu zilizokusanywa na Wizara ya Usalama wa ndani zinaonyesha kuwa jumla ya lita 2,846,590 za pombe haramu zimenasa kote nchini tangu Disemba 2025, huku washukiwa wasiopungua 973 wakikamatwa katika operesheni inayoendeshwa na mashirika mbalimbali ya usalama.
Kwa mtazamo wa kikanda, Bonde la Ufa linaongoza kwa zaidi ya lita 870,000 zilizonaswa.
Nyanza inafuatia kwa zaidi ya lita 690,000, huku Magharibi mwa Kenya ikiwa na lita 600,000, jambo linalothibitisha kuwa maeneo haya yanaongoza katika biashara hiyo haramu.
Maafisa wa usalama wanasema maeneo haya yana historia ndefu ya utengenezaji wa pombe za kienyeji kama busaa na changáa.
Garissa ilirekodi lita 60 pekee, Wajir lita 108 kisha Nyandarua lita 515, huku Makueni, Tana River na Kajiado pia zikiwa na takwimu za chini.