Watoto miongoni mwa 12 walioshtakiwa kwa kushiriki maandamano ya mafuta
WAANDAMANAJI kumi na wawili, wakiwemo watoto wawili, Jumatano, Aprili 22, 2026 walifikishwa mahakamani wakishtakiwa kwa kushiriki maandamano ya kutaka serikali kupunguza bei ya mafuta mnamo Jumanne.
Washtakiwa kumi watu wazima walikanusha mashtaka yaliyowasilishwa dhidi yao na Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma mbele ya Hakimu wa Mahakama ya jiji la Nairobi.
Wakili wa washtakiwa, Ian Mutiso, aliomba washitakiwa waachiliwe kwa dhamana akisema kosa linalowakabili ni dogo na halina adhabu kali.
“Washtakiwa wanakabiliwa na mashtaka kwa kutekeleza haki zao za kikatiba. Kwa wakati ufaao, nitapinga uhalali wa mashtaka haya,” alisema Mutiso.
Aidha, aliomba watoto hao wawili wapelekwe katika kituo cha afya ili kufanyiwa uchunguzi kubaini umri wao.
Upande wa mashtaka haukupinga ombi la dhamana.
Washtakiwa hao wanakabiliwa na kosa la kuzuia kwa makusudi matumizi huru ya barabara za umma, kinyume na Kifungu cha 11(1)(a) kikisomwa pamoja na Kifungu cha 11(2) cha Sheria ya Usumbufu wa Umma ya Kaunti ya Nairobi ya mwaka 2021.
Katika uamuzi, Hakimu Mkuu Mwandamizi Roda Yator aliwaachilia washtakiwa kwa dhamana ya pesa taslimu ya Sh3,000 kila mmoja.
Pia aliamuru Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Central awasindikize watoto hao hadi katika kituo cha afya kutathminiwa umri wao.
Kesi hiyo itatajwa Mei 7, 2026 na kutengewa tarehe ya kusikilizwa.