Habari

Natembeya akosoa msako dhidi ya magenge katika kaunti yake

Na EVANS JAOLA April 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 2

GAVANA wa Kaunti ya Trans Nzoia, George Natembeya anazozana vikali na maafisa wa usalama kutokana na operesheni inayoendelea dhidi ya magenge ya wahalifu katika mji wa Kitale, akidai kuwa msako huo unatumika kisiasa na unalenga vijana pamoja na wafuasi wake.

Operesheni hiyo, ambayo sasa inaingia wiki ya pili, iliagizwa na Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen, ambaye aliagiza Inspekta Jenerali wa Polisi kupeleka kikosi maalum ili kukabiliana na ongezeko la uhalifu katika kaunti hiyo.

Murkomen alisema hatua hiyo ni muhimu kurejesha amani, akisisitiza kuwa serikali haitaruhusu magenge kudhibiti eneo lolote nchini.

Hata hivyo, Gavana Natembeya amepinga vikali operesheni hiyo, akiitaja kama “isiyo halali na ya ubaguzi.”

Alidai kuwa polisi wanawalenga vijana kiholela na kuwakamata watu wasiohusika na uhalifu, akionya kuwa hali hiyo inaleta hofu miongoni mwa wakazi wa Kitale.

“Kinachoendelea hapa si haki. Ni matumizi ya nguvu ya polisi kwa malengo ya kisiasa,” alisema.

Kauli hiyo imepingwa na maafisa wa usalama. Mkuu wa Upelelezi wa Jinai wa kaunti, Josephat Ndung’u, alisema operesheni hiyo ni ya kisheria.

Ndung’u alikanusha uwepo wa kafyu yoyote Kitale, akisema taarifa hizo ni kupotosha zinazoenezwa na wahalifu ili kuwatisha wananchi.

Alisisitiza kuwa operesheni inalenga kurejesha utulivu na si kulenga watu kwa misingi ya kisiasa.

Kwa mujibu wa polisi, zaidi ya watu 170 wamekamatwa katika wiki ya kwanza ya msako huo, wakiwemo mahabusu watano waliotoroka rumande.

Kamanda wa Polisi wa Kaunti Riko Ngare, alisema msako umefanywa katika maeneo kama Tuwan, Matisi, Mitume, Kipsongo na Namanjalala.

Polisi pia walisema wamenasa bidhaa mbalimbali zinazodaiwa kuwa za wizi, zikiwemo zaidi ya simu 200, laptopu na mitungi ya gesi.

Ngare alisema uchunguzi umebaini uwepo wa mtandao wa wizi wa simu unaounganisha Kitale na maeneo ya Kapenguria na Lodwar, akionya kuwa mtandao huo ni mpana zaidi ya ilivyodhaniwa awali.

Aidha, polisi wamedai baadhi ya magenge hayo yanafadhiliwa na wanasiasa kwa lengo la kuwatisha wapinzani na kuimarisha ushawishi wa kisiasa.

Kauli hizo zimezua mjadala mkali kuhusu uhusiano kati ya siasa na uhalifu katika eneo hilo.

Hata hivyo, mashirika ya haki za binadamu, ikiwemo Justice and Peace Centre Kitale, yameeleza wasiwasi kuhusu madai ya matumizi kupita kiasi ya nguvu.

Afisa wa shirika hilo, Bonface Wanyonyi, alisema baadhi ya wakazi wamelalamika kuhusu hofu, kukamatwa kiholela na unyanyasaji unaodaiwa kufanyika wakati wa operesheni.

Kamishna wa Kaunti, Gideon Oyagi, amewataka wanasiasa kujiepusha na kufadhili au kuhifadhi magenge ya uhalifu, akionya kuwa yeyote atakayehusika atachukuliwa hatua kali za kisheria.