Vyama vya kisiasa vyageuza wawaniaji ‘ng’ombe’ wa kukamuliwa pesa
VYAMA vikuu vya siasa nchini vimeanza kukusanya mamilioni ya pesa kutoka kwa wawaniaji wanaotafuta tiketi za uchaguzi mkuu wa 2027, katika hali inayojitokeza kama njia mpya ya mapato yenye faida kubwa kwa vyama hivyo.
Tofauti na ilivyokuwa hapo awali, ambapo ada zilitozwa wakati wa uteuzi wa wagombeaji pekee, sasa baadhi ya vyama vinatoza ada ya hadi Sh50,000 kwa mtu anayeonyesha tu nia ya kugombea kwa tiketi yao.
Hatua hii imezua mjadala kuhusu iwapo vyama vinageuza siasa kuwa biashara badala ya kuwa jukwaa la uwakilishi wa wananchi.
Chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP) kinachohusishwa na aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua ni miongoni mwa vyama vilivyoanza mwelekeo huu.
Kupitia kwa notisi iliyotolewa Jumatano, chama hicho kiliwataka wawaniaji kujisajili mapema ili kushiriki katika uchaguzi ujao.
Kwa mujibu wa notisi hiyo, wanaotaka kugombea ugavana wanatakiwa kulipa Sh50,000 kama ada ya usajili, huku wanaowania useneta, ubunge na uwakilishi wa kike wakitakiwa kulipa Sh10,000.
Wanaowania viti vya udiwani watalipa Sh5,000, huku vijana na wanaoishi na ulemavu wakipunguziwa ada kwa nusu.
Katibu Mkuu wa DCP, Hezron Obaga, alitetea ada hizo akisema zinalenga kubaini wawaniaji walio na dhamira ya dhati.
“Tumelazimika kuweka ada ndogo ili kutambua wale walio makini na waliojitolea kuwania kupitia chama chetu na waliojitokeza wamekuwa wengi,” alisema.
Hatua hiyo inajiri mwezi mmoja baada ya Rais William Ruto kupitia chama cha United Democratic Alliance (UDA) kukusanya zaidi ya Sh31 milioni kutoka kwa wawaniaji 12,353 waliohudhuria mkutano wa wawaniaji uliofanyika Ikulu.
Kati ya kiasi hicho, wawaniaji wa udiwani walilipa Sh2,000 kila mmoja na kuchangia zaidi ya Sh20 milioni.
Wanaotaka ugavana walilipa Sh10,000 kila mmoja na kutoa jumla ya Sh1.49 milioni, huku wanaowania ubunge, useneta na uwakilishi wa kike wakilipa Sh5,000 kila mmoja na kuchangia karibu Sh9.8 milioni.
Chama cha ODM pia kimetangaza mipango ya kufungua usajili wa wawaniaji, ingawa hakijaweka wazi kiwango cha ada kitakachotozwa.
Kwa kawaida, ada za uteuzi katika vyama vikuu bado ni kubwa, zikifikia hadi Sh500,000 kwa wagombea ugavana, Sh250,000 kwa ubunge, useneta na uwakilishi wa kike, huku wanaowania udiwani wakitozwa takriban Sh50,000.
Mbali na ada zinazotolewa na wawaniaji, vyama vya siasa hupokea fedha kutoka kwa hazina ya umma kupitia Hazina ya Vyama vya Siasa.
Zaidi ya Sh7 bilioni tayari zimetolewa kwa vyama tangu mwaka wa 2013, hatua inayochangia kufanya vyama kuwa shughuli yenye faida kubwa.
Hata hivyo, licha ya mgao huo mkubwa wa fedha za umma, vyama vingi hubaki kuwa butu nje ya vipindi vya uchaguzi, bila shughuli madhubuti mashinani.
Lakini uchaguzi unapokaribia, vyama vipya huibuka huku vile vilivyokuwapo vikifufuliwa upya.
Kwa mujibu wa Msajili wa Vyama vya Siasa, John Cox Lorionokou, Kenya kwa sasa ina vyama 92 vilivyosajiliwa kikamilifu, huku vingine 34 vikipata usajili wa muda katika miezi ya hivi majuzi.
“Katiba yetu inaruhusu mfumo wa vyama vingi na haki za kisiasa kwa Wakenya wote. Hakuna kiwango cha juu kilichowekwa kuhusu idadi ya vyama,” alisema Lorionokou.
Aliongeza kuwa kuongezeka kwa uhamasishaji kuhusu haki za kisiasa na hitaji la kupanua nafasi ya kidemokrasia kumechangia ongezeko hilo.
Hata hivyo, wachambuzi wanasema kuwa ongezeko la vyama pia linachochewa na hofu miongoni mwa wanasiasa kunyimwa tiketi katika vyama vikuu, hali inayowasukuma kuanzisha vyama vipya au kuhamia kwa vile vidogo ili kuongeza nafasi zao za kushiriki uchaguzi.
Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa pia yamechangia kuanzishwa kwa vyama vingi.
Sheria hiyo inaeleza kuwa asilimia 70 ya fedha hugawiwa kwa misingi ya kura zilizopatikana, asilimia 15 kwa kuzingatia uwakilishi wa makundi maalum, asilimia 10 kulingana na idadi ya viongozi waliochaguliwa, huku asilimia tano ikitengwa kwa matumizi ya kiutawala ya ofisi ya msajili.
Kwa sasa, vyama vipya kama National Forum Party (NFP), Clean Alliance Party of Kenya (CAP-K), New Face Party of Kenya (FACE) na Mwongozo Mpya Party (MMP) vimejitokeza, kuonyesha wazi kuwa ushindani wa kisiasa kuelekea 2027 umeanza mapema.
Kadri siasa zinavyozidi kupamba moto, mzigo wa kifedha unaonekana kubebwa zaidi na wawaniaji, hali inayozua maswali kuhusu usawa wa kisiasa na iwapo mfumo huu unawanyima nafasi wale wasio na uwezo mkubwa wa kifedha kushiriki kikamilifu katika uongozi wa nchi.