Kinachofanya Wabunge kukwama na Mswada wa ushirikishaji Umma
BUNGE linaendelea kujadili masuala yanayohusu Mswada wa Ushirikishaji wa Umma wa mwaka 2025, huku wabunge wakikabiliana na angalau hoja sita zenye utata kabla ya kuupitisha kuwa sheria kamili.
Mswada huo, unaofadhiliwa na Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo na mwenzake wa Ainabkoi Samuel Chepkonga, tayari umepita hatua ya Kusomwa Mara ya Pili na sasa unaelekea katika kikao cha wabunge wote, ambapo marekebisho yatajadiliwa.
Lengo kuu la mswada ni kuweka mfumo rasmi wa kuhakikisha wananchi wanashirikishwa kikamilifu katika utungaji na utekelezaji wa sera za umma, kwa kuzingatia Katiba inayotambua kuwa mamlaka ya mwisho yapo mikononi mwa wananchi.
Hata hivyo, wabunge wanakumbana na changamoto kadhaa zitakazoamua hatma ya sheria hiyo.
Miongoni mwa masuala yanayojadiliwa ni iwapo wananchi wanaoshiriki mikutano ya kukusanya maoni ya umma wanapaswa kulipwa au wachukulie jukumu hilo kama wajibu wa kiraia sawa na kupiga kura.
Pia, kuna mjadala kuhusu iwapo ianzishwe hazina maalum ya kufadhili shughuli za ushirikishaji wa umma, idadi ya watu wanaopaswa kushirikishwa, namna ya kurekodi na kuzingatia maoni ya wananchi, muda wa kutoa taarifa kabla ya mikutano, na muda unaofaa kwa mchakato huo.
Bunge linachukua tahadhari kubwa baada ya mahakama hapo awali kubatilisha sheria kadhaa kwa kukosa ushirikishaji wa umma wa kutosha.
Mwaka 2014, aliyekuwa Jaji wa Mahakama Kuu, George Odunga, alisisitiza kuwa ushirikishaji wa umma si jambo la kupamba tu bali ni sehemu muhimu ya mchakato wa kutunga sheria.
Kutokuwepo kwa sheria maalum kumesababisha tafsiri tofauti mahakamani kuhusu ubora na kiwango cha ushirikishaji wa umma.
Katika vikao vya kusikiliza maoni ya wananchi, Kamati ya Haki na Masuala ya Kisheria ilikumbana na changamoto za kiutendaji.
Kwa mfano, mkazi mmoja wa Kajiado alisema alisafiri karibu kilomita 400 kuhudhuria kikao na alihitaji kufidiwa gharama zake.
Mwakilishi wa Wanawake wa Lamu Muthoni Marubu alieleza kuwa wananchi wengi hutumia kati ya Sh1,000 na Sh2,000 kufika kwenye mikutano hiyo, na hivyo ni haki kufidiwa.
Hata hivyo, baadhi ya wabunge wameonya kuwa hatua hiyo inaweza kutumiwa vibaya na pia kuwa vigumu kupanga bajeti kutokana na idadi isiyotabirika ya washiriki.
Mbunge wa Kibwezi Magharibi Mwengi Mutuse alisema wananchi wengi wamependekeza kuwe na fedha maalum za kugharamia ushirikishaji huo, lakini hoja hiyo bado inazua mjadala mkali.
Dkt Amollo alionya kuwa ingawa kulipa washiriki kunaweza kuwa maarufu, kuna hatari zake. Alisema taasisi nyingi tayari zinakabiliwa na upungufu wa bajeti na zinaweza kushindwa kugharamia shughuli hizo ipasavyo.
Mbunge wa Gatanga Edward Muriu alitaka kuwepo kwa mfumo wazi wa kupima ubora na idadi ya ushirikishaji wa umma, akieleza kuwa mara nyingi maoni ya wananchi hubadilishwa kabla ya kufikishwa bungeni.
Naye Mbunge wa Tetu Geoffrey Wandeto alisema tafsiri zisizoeleweka za maneno kama “ya kutosha” na “yenye maana” zimechangia kufeli kwa sheria nyingi, akitaka yawekwe wazi ili kuepuka kesi zisizoisha mahakamani.
Aidha, wabunge wanajadili iwapo mikutano hiyo inafaa kufanyika katika ngazi ya maeneo bunge au wadi, huku Mbunge wa Kabondo Kasipul Eve Obara akionya kuwa taratibu nyingi zinaweza kuchelewesha maamuzi na kutumia rasilimali nyingi.
Mwakilishi wa Wanawake wa Uasin Gishu Gladys Boss amepinga pendekezo la kuwaadhibu kisheria maafisa watakaoshindwa kufuata taratibu za ushirikishaji wa umma.
Kifungu hicho kinapendekeza faini ya hadi Sh500,000 kwa maafisa kama Mwanasheria Mkuu, Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma, makarani wa mabunge na magavana.
Bi Boss alionya kuwa adhabu hizo zinaweza kuwaathiri maafisa hao na kuathiri utendaji kazi, hasa pale majukumu yanapokabidhiwa wengine.
Maelezo ya ziada: Benson Matheka