Habari za Kitaifa

Watu 11 wakamatwa maandamano ya kupinga bei za mafuta; taharuki yatanda miji kadhaa

Na WAANDISHI WETU April 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WATU kadhaa walikamatwa Jumanne, Aprili 21, baada ya maandamano ya kulalamikia kupanda kwa bei ya mafuta kushuhudiwa katika maeneo mbalimbali nchini, huku hali ya taharuki ikiripotiwa katika miji kadhaa.

Kamanda wa Polisi wa Kanda ya Nairobi, Issa Mohamud, alithibitisha kuwa watu 11 walikamatwa katika eneo la Katikati ya Jiji baada ya kuandamana akisisitiza hawakuwa na kibali.

Akizungumza na wanahabari alipokagua hali katika jijini, Mohamud alisema hali ilikuwa shwari huku zaidi ya asilimia 98 ya biashara zikiendelea na shughuli kama kawaida.

“Hadi sasa tumewakamata 11 na watafikishwa mahakamani kesho,” alisema, akiongeza kuwa hakukuwa na sababu ya wananchi kuwa na hofu.

Hata hivyo, biashara nyingi zilifungwa kwa hofu ya kuvamiwa na wahuni huku taharuki ikitanda jijini.

Bw Mohamud aliwataka wafanyabiashara waliokuwa wamefunga maduka kwa hofu ya vurugu kurejelea shughuli zao, akisisitiza kuwa polisi walikuwa macho kuhakikisha amani inadumishwa.

Mwandamanaji akinyanyuliwa na kutupwa kwenye karandinga la polisi eneo la Archives, katikati ya jiji la Nairobi. Polisi walisema maandamano ya kupinga bei za mafuta ni haramu kwa sababu hayana kibali. Picha|Billy Ogada

Maandamano hayo yalichochewa na wito uliosambaa mitandaoni, ambapo vijana walilalamikia ongezeko la bei ya mafuta lililotangazwa na Mamlaka ya Kudhibiti Nishati na Petroli (EPRA).

Wengi walilalamikia kupanda kwa gharama ya maisha, wakisema bei ya usafiri, chakula na bidhaa muhimu imekuwa ghali kupita kiasi.

Katika jiji la Nairobi, idadi ya waandamanaji ilikuwa ndogo ikilinganishwa na maandamano ya awali, huku polisi wakidhibiti hali mapema na kuwatawanya waliokuwa wamekusanyika.

Huko Embu, hali ilikuwa tofauti ambapo mamia ya vijana walijitokeza barabarani na kusababisha vurugu.

Walichoma magurudumu, kufunga barabara na kulazimisha wafanyabiashara kufunga maduka yao kwa hofu ya kuporwa.

Polisi waliwasili na kuwaamuru watawanyike lakini walikaidi, hali iliyosababisha mapambano makali kati yao na maafisa wa usalama.

Mji huo uligeuka kuwa mahame huku wakazi na wafanyabiashara wakihepa.

Katika mji wa Kiritiri, Mbeere Kusini, vijana walifunga barabara ya Embu–Kiritiri kwa na kusababisha msongamano mkubwa wa magari.

“Ongezeko la bei ya mafuta linafanya maisha ya Wakenya kuwa magumu zaidi,” alisema mmoja wa waandamanaji.

Katika mji wa Kitengela, hali ya taharuki pia iliripotiwa huku makundi ya vijana wakiongozwa na kiongozi wa kundi la Free Movement, Bob Njagi, wakiingia barabarani kulalamikia bei ya mafuta. Walisimamisha usafiri kwenye Barabara ya Namanga na kabla ya kutawanywa kwa kutumia vitoa machozi.

Wafanyabiashara wengi walifunga maduka yao kwa hofu ya uporaji, hali iliyofanya mji huo kuonekana kutelekezwa kwa muda.

Maduka makubwa pia yalifungwa licha ya uwepo wa polisi wengi na hata doria za angani.

Kamanda wa Polisi wa Isinya, Simon Lokitari, alisema maafisa wa polisi waliovalia sare na wale wa kiraia walitumwa kuhakikisha usalama.

“Maafisa wa usalama wako macho kulinda biashara na kuhakikisha usafiri hautatiziki. Tunawatafuta waandalizi wa maandamano haya ili wachukuliwe hatua za kisheria,” alisema.

Katika mji wa Karatina, kaunti ya Nyeri, waandamanaji walikabiliana vikali na polisi waliokuwa wakijaribu kuwatawanya baada ya kufunga barabara.

Hata hivyo katika miji ya Pwani, Bonde la Ufa, Nyanza na Magharibi hakukuwa na maandamano.