Jamvi La Siasa

Karua awaka, ahusisha sera za Ruto na masaibu ya wakulima wa chai

April 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Kiongozi wa People’s Liberation Party (PLP) Martha Karua amemkosoa vikali Rais William Ruto kuhusu sera yake ya mambo ya nje, akiihusisha na changamoto za kiuchumi zinazowakumba wakulima wa chai katika eneo la Mlima Kenya.

Katika taarifa aliyotoa Ijumaa, Aprili 24, 2026, Karua alishutumu serikali kwa kuendesha diplomasia  kiholela, hasa kwa kuhusiana na kundi la Rapid Support Forces (RSF) linalopigana Sudan, akidai hali hiyo imeathiri uhusiano wa kibiashara na kuwaumiza wakulima wa humu nchini.

“Sudan, ambayo ni miongoni mwa wanunuzi wakuu wa chai mnayozalisha, ilipotangaza kusitisha kwa muda usiojulikana uagizaji wa bidhaa kutoka Kenya mwezi uliopita, ni nyinyi mlioathirika—na bado mnaendelea kuathirika. Familia zenu sasa zinahangaika jinsi ya kulipa karo, na haya yote ni matokeo ya mvutano wa kidiplomasia na majirani zetu,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.

Karua alisema athari hizo zilianza kujitokeza wazi baada ya Sudan, soko muhimu la chai ya Kenya, kusitisha uagizaji huo, hali iliyowaacha wakulima wakikabiliana na hasara.

Alieleza kuwa kabla ya marufuku hiyo, Sudan ilikuwa ikiagiza zaidi ya kilo 10.7 milioni  za chai ya Kenya kila mwaka, ikiingiza kati ya Sh3.88 bilioni na Sh5.17 bilioni. Kusimamishwa kwa biashara hiyo, alisema, kunaweza kusababisha hasara ya hadi Sh7 bilioni katika sekta hiyo.

Karua aliendelea  kudai kuwa hatua hiyo ya Sudan inahusishwa na madai ya Kenya kuwa na uhusiano na watu wanaohusishwa na RSF. Alirejelea wasiwasi ulioibuliwa mapema mwaka huu kuhusu ripoti kwamba Algoney Hamdan Dagalo—ndugu wa kamanda wa RSF Hamdan ‘Hemedti’ Dagalo—alipewa pasipoti ya Kenya.

“Ni janga la uongozi. Wakati Ruto anazunguka nchi akidai anaungwa mkono kwa wingi katika Mlima Kenya, sera zake zinapunguza kipato cha watu anaodai kuwajali,” aliandika.

Kiongozi huyo wa PLP pia aliikosoa serikali kwa kuchelewesha mradi wa upanuzi wa Bwawa la Thiba, akisema hali hiyo imeathiri pakubwa wakulima wa Mwea. Alinukuu ripoti ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Umma iliyoonyesha kuwa zaidi ya Sh42 milioni za walipa ushuru zilipotea kutokana na faini za riba kufuatia kucheleweshwa kwa malipo kwa wakandarasi.

“Wanapopoteza zaidi ya Sh40 milioni kwa adhabu badala ya kukamilisha mitaro ya  unyunyuzaji, wanapora mustakabali wa watoto wenu,” alisema Karua.

Bi Karua alishtumu serikali ya Kenya Kwanza kwa kushindwa kusaidia sekta muhimu za kilimo, akisema wakulima wa chai, kahawa na mpunga wameachwa bila msaada unaohitajika.

Karua alitoa wito wa uwazi zaidi katika sera za nje za serikali na kusisitiza haja ya hatua za haraka kuimarisha sekta ya kilimo na kulinda masoko ya nje.