Habari za Kitaifa

Makubaliano ya siri yaliyomaliza tandabelua kati ya maseneta na magavana

Na NDUBI MOTURI April 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAKUBALIANO ya siri kati ya magavana na maseneta yalimaliza mvutano wa wiki kadhaa uliotishia kufifisha shughuli za kaunti kutokana na kucheleweshwa kwa fedha.

Katika makubaliano hayo, magavana wamekubali kufika mbele ya kamati za Seneti kwa ukaguzi wa matumizi ya fedha, kuachana na takwa la kuondolewa kwa maseneta wanne katika kamati hiyo na kusitisha mashambulizi ya hadharani dhidi ya seneti.

Kwa upande wao, maseneta wameahidi kushughulikia madai ya ulaghai na ubadhirifu wa kifedha kwa mujibu wa taratibu zao za ndani, kudumisha nidhamu katika kamati na kuzingatia uwezekano wa kuongeza mgao wa fedha kwa kaunti.

Makubaliano hayo yalifikiwa baada ya mazungumzo ya muda mrefu faraghani yaliyofanyika Seneti yakiongozwa na Kiongozi wa Wengi Aaron Cheruiyot na ujumbe wa Baraza la Magavana ukiongozwa na mwenyekiti wake Ahmed Abdullahi.

Mdokezi aliyehudhuria kikao hicho anasema mazungumzo yalikuwa makali, huku kila upande ukishikilia msimamo kabla ya kufikia mwafaka.

“Kulikuwa na mvutano mkubwa. Magavana walitaka kuhakikishiwa heshima katika vikao, huku maseneta wakitaka ushirikiano kamili. Mwishowe kila upande ulikubali kupunguza makali,” alisema.

Kwa mujibu wa makubaliano hayo, magavana sasa wataanza tena kufika mbele ya Kamati ya Matumizi ya Kaunti, hatua inayokomesha kususia kwao kulikosababisha magavana 29 kukataa kuitikia wito wa Seneti na hata kuibua vitisho vya kukamatwa kwao.

Kwa upande wao, maseneta wamekubali kushughulikia madai ya ulaghai na kuhakikisha vikao vinaendeshwa kwa heshima.

Pia, uongozi wa Seneti umeahidi kuwasihi wanachama wa kamati kupunguza lugha kali wakati wa vikao, moja ya malalamishi makuu ya magavana.

Seneta wa Mandera Ali Roba, aliyekuwa sehemu ya kikosi cha upatanishi, aliambia Bunge kuwa maslahi ya Seneti yalilindwa ipasavyo.

Mswada wa Ugavi wa Mapato uliibuka suala nyeti katika mazungumzo hayo, huku magavana wakionya kuwa kucheleweshwa kwake kunaweza kulemaza utoaji wa huduma katika kaunti.

Hata hivyo, licha ya muafaka huo, mgawanyiko ndani ya Seneti uliibuka wazi wakati mswada huo ulipowasilishwa.

Seneta wa Migori Eddy Oketch alipinga hatua hiyo akisema seneti ilipaswa kwanza kusuluhisha mzozo huo kikamilifu.

Seneta wa Laikipia John Kinyua naye alilalamika kuwa maseneta hawakushirikishwa katika mazungumzo hayo, huku Seneta Agnes Kavindu akitaka kufanyika kwa kikao cha ndani kwanza kabla ya kuendelea na mjadala kuhusumswada huo.

Mvutano huo ulizua vurugu ndani ya seneti hadi Spika Amason Kingi akalazimika kuahirisha kikao ili kutoa nafasi ya mashauriano.

Baadaye, baadhi ya maseneta walitoka nje wakilalamika.

Licha ya makubaliano hayo kuruhusu kuendelea kwa vikao vya ukaguzi na mijadala ya miswada muhimu, hali ndani ya Seneti inaonyesha kuwa bado kuna tofauti.

Chanzo kimoja kilisema, “Huu haukuwa mwisho wa mzozo, bali ni hatua ya kusonga mbele huku tofauti zikiendelea kushughulikiwa.”

Mvutano huo ulianza baada ya magavana kususia vikao vya Seneti wakidai kunyanyaswa kisiasa, hali iliyosababisha Seneti kusitisha mijadala ya miswada muhimu ya fedha na hata kutishia hatua kali dhidi ya waliokaidi.