Habari za Kitaifa

‘Nusura watuue’: Manusura wa utekaji nyara wasimulia kufanyiwa ukatili wa kutisha

Na STEVE OTIENO June 30th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

WAATHIRIWA saba wa utekaji nyara waliotoweka baada ya kukamatwa katika maadhimisho ya pili ya maandamano ya kupinga Mswada wa Fedha wa 2024, mnamo Juni 25, jana walisimulia masaibu waliyokumbana nayo mikononi mwa polisi.

Wote saba walikusanyika Nairobi kuadhimisha maandamano ya Gen-Z yaliyobadilisha mkondo wa siasa nchini.

Baadhi yao waliweka mashada ya maua nje ya majengo ya bunge kuwakumbuka waliouawa katika maandamano ya mwaka jana kabla ya polisi kuwatawanya.

Kutokana na masimulizi yao ya kutisha, kilichofuata kilitofautiana kabisa na kukamatwa kwa njia halali.

Davis Lichuma ni mwanaharakati wa mwisho kupatikana miongoni mwa saba waliotoweka baada ya kukamatwa wakati wa maandamano yaliyofanyika jijini Nairobi, Alhamisi.

Kwa karibu siku nne, familia yake ilimtafuta katika vituo vya polisi, hospitali na mochari.

Waliompata waliripotiwa kusema alikuwa amelala kando ya barabara, akiwa amechanganyikiwa wala hangeweza kuzungumza.

Waendeshaji bodaboda walipomsafirisha katika kitengo cha dharura cha Hospitali ya Kenyatta (KNH) Jumapili usiku, hawakuwa na habari kuwa wamemwokoa mmoja kati ya watu waliotoweka ambaye alitafutwa sana.

Mwendo wa saa tatu unusu usiku, kaka yake mkubwa, Benson Shikala, akifuata alichotaja kuwa dhamiri au nafsi yake, aliamua kujaribu mara ya mwisho kumtafuta KNH.

“Niliambiwa watu wengi walifika hapo na nilipotazama, niliona mtu akiwa uchi, lakini alikuwa na rasta kama kaka yangu. Nilisogea karibu na nikamtambulisha,” alisimulia Bw Shikala.

“Alikuwa na njaa sana, amepagawa, hakusikia chochote na ungemgusa, alitaka kutoroka. Alijaa hofu na hakumjua yeyote. Alichanganyikiwa kabisa.”

Kupatikana kwake kulifikisha kikomo siku kadhaa zilizojaa mahangaiko na wasiwasi kwa familia na wenzake lakini zikafungua ukurasa wa kutatiza zaidi, huku wahanga wakisimulia mateso, kuzuiliwa kisiri na vitisho walivyodai kupitia waliposhikwa mateka.

Sawia na Lichuma, wenzake sita walitupwa kando ya barabara ya Ngong.

Frederick Ojiro Odhiambo alisimulia jinsi maafisa waliovalia kiraia waliwakamata nje ya majengo ya bunge kabla ya kuwarundika kwenye gari la polisi mwendo wa saa tano asubuhi na kuendeshwa kwa kasi kuelekea Kituo cha Polisi cha Nairobi Central.

“Tulifikiri tunapelekwa hapo,” akasema.

Badala yake, maafisa wawili waliabiri, wakaingia kituoni na kurejea kisha gari likaondoka tena.

Msafara huo baadaye ulisimama nje ya Kituo cha Polisi cha Parklands ambapo afisa mwengine alishuka, akapiga simu kadhaa na kurejea.

Kutoka hapo, gari lilielekea mbele ya Limuru kuelekea barabara kuu ya Naivasha-Nakuru, huku wanaharakati waliochanganyikiwa ndani ya gari wakigubikwa na hofu.

Christine Lubanga alikumbuka kusafiri pamoja na maafisa wanane wa polisi kwa karibu nusu saa kabla ya lori kusimama eneo lisilojulikana kando ya barabara kuu.

Kabla ya yeyote kuwasiliana na jamaa au wakili, msafara mwingine uliwasili.

“Subaru tatu ziliwasili na tukarushwa ndani ya buti wawili wawili,” akasema Collins Otieno anasema waliagizwa kutoka kando ya barabara kabla ya wanaume waliojihami kuwashurutisha waingie magari yaliyowasubiri.

“Walituelekezea bunduki, wakitueleza tusidhubutu kukimbia. Nilichukuliwa nikipigwa na kulazimishwa kuingia buti. Simu zetu zilitwaliwa na hatujaziona tena,” akasema.

Safari hiyo iliishia katika nyumba ya mahame ndani ya msitu, walisema waathiriwa hao.

Wanaharakati hao wanadai siku zilizofuata walistahimili kushambuliwa wakiwa wamefunikwa macho na kuzuiliwa wakiwa wametenganishwa.

Kulingana na ushuhuda wao, walitandikwa, wakapigwa mateke na kudhalilishwa kimwili.

Watetezi wa haki za kibinadamu waliokutana nao baada ya kuachiliwa walisema kadhaa walipata majeraha yanayohitaji matibabu.

Michael Ngige, almaarufu kama “Jomo Kenyatta Junior”, alifanyiwa uyoka (CT scan) baada ya kulalamika kuhusu maumivu mwilini mwake.

Kulingana na Mkurugenzi wa Shirika la Vocal Africa, Hussein Khalid, wanaharakati walisema waliowahoji walitaka kujua ni nani aliyewafadhili na ni wapi walitoa kamera za kubandika mwilini walizotumia kurekodi tabia ya polisi wakati wa maandamano.

Kwa familia, tukio hilo limeacha makovu yanayozidi majeraha ya mwili waliyopata wapendwa wao.

Mashirika ya kutetea haki yanasema kupatikana kwa wanaharakati hao saba hakuashirii mwisho wa kero hilo.

Bw Khalid alisema watu wengine kadhaa walioripotiwa kutoweka siku chache kabla ya maandamano wiki iliyopita, bado hawajulikani walipo, wakiwemo Macmillan Kiarie na Abdulaziz Duba.

Mwanaharakati Boniface Mwangi ameitisha uwajibikaji akisisitiza ikiwa walitenda uhalifu, washukiwa walistahili kushtakiwa kwa njia halali badala ya kutoweka.