Korti yatoa amri ya 3 kuzima ujenzi wa Ikulu msituni
MAHAKAMA ya Mazingira na Ardhi ya Meru jana ilitoa amri ya tatu ya kusitisha kutengwa kwa sehemu ya ardhi ya Msitu wa Imenti kwa ajili ya ujenzi wa Ikulu-ndogo ya Rais.
Serikali inalenga miradi mingine ikiwemo kujenga uwanja wa gofu na ule ndege msituni humo.
Mahakama ilichukua hatua hiyo kufuatia kesi iliyowasilishwa na mashirika yanayohusika na uhifadhi wa mazingira.
Jaji Oguttu Mboya jana alitoa amri ya muda kutokana na kesi zilizowasilishwa na Mashirika ya Pan African Climate Justice Alliance (PACJA) na Meru Forest Conservation Forum.
Mahakama pia iliongeza muda wa amri zilizotolewa Juni 10 katika kesi iliyowasilishwa na mwanaharakati Francis Awino hadi Juni 30 wakati kesi hiyo itakapotajwa tena mahakamani.
Amri zote mbili za muda zitaendelea kutekelezwa hadi kesho, ambapo kesi nyingine iliyowasilishwa na wakazi watano wa Meru na kuungwa mkono na Chama cha Mazingira Green itatajwa mahakamani.
Jaji Mboya alisema mahakama inatarajiwa kuunganisha kesi hizo na kuzishughulikia pamoja.
Mahakama pia inatarajiwa kusikiliza ombi la kudharau mahakama lililowasilishwa na Bw Awino dhidi ya Mwanasheria Mkuu, Waziri wa Mazingira, Shirika la Misitu Nchini (KFS), Tume ya Kitaifa ya Ardhi (NLC) na Maspika wa Seneti na Bunge la Kitaifa.
Waliojumuishwa katika kesi hiyo wamepewa siku saba kujibu madai hayo ya kudharau mahakama.
Wakili wa Serikali Eric Obura, aliyewakilisha mwanasheria mkuu, waziri wa mazingira na KFS, aliiambia mahakama kuwa serikali imezingatia kikamilifu amri zilizotolewa.
“Bado sijawasilisha majibu kuhusu ombi la dharau kwa sababu tulikabidhiwa nyaraka hizo Ijumaa alasiri. Naiomba mahakama itupe siku saba kujibu. Hata hivyo, msimamo wetu ni kwamba msitu bado uko salama na hatujakiuka amri za korti,” akasema Bw Obura.
Katika kesi ya kwanza, Bw Awino pia anataka mahakama iamuru kutolewa kwa nyaraka zote zinazohusiana na miradi inayopendekezwa ndani ya msitu wa Imenti.
Mwanaharakati huyo wa haki za binadamu pia anataka mahakama kufuta maamuzi yote yaliyofanywa hadi sasa kuhusu kutenga sehemu ya msitu kwa ajili ya miradi inayokusudiwa.
Katika kesi ya pili, Mugambi Imanyara, Charles Mutuma, Mwenda Kirera, Michael Koome na Douglas Mwiti wanadai kuwa miradi inayolengwa inahatarisha uwepo wa msitu huo.