IEBC: Vijana wamejisajili kwa fujo kushiriki kura, hatujaona ufanisi kama huu awali
TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) imesajili zaidi ya wapigakura milioni 2.6 baada ya kufungwa kwa shughuli ya uandikishaji Jumanne, hatua kubwa katika maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Kulingana na ripoti ya mwisho kuhusu shughuli hiyo, iliyotolewa na Tume jana, jumla ya wapigakura 2,612,725 wamesajiliwa kupitia mikumbo miwili sambamba.
Kati ya hao, wapigakura 267,249 walisajiliwa chini ya usajili wa kawaida uliofanywa katika ofisi za IEBC kati ya Septemba 29, 2025 na Aprili 2026.
Idadi kubwa, wapigakura 2,345,476, waliongezwa kwenye sajili wakati wa awamu ya usajili wa wengi kati ya Machi 30 na Aprili 28, 2026.
Katika mwezi huo mmoja, usajili ulifanyika katika maeneobunge yote 290 na wadi 1,450, katika Vituo vya Huduma Centre, taasisi za elimu ya juu, na Kituo cha Huduma kwa Wateja cha IEBC, Nairobi, na hivyo kurahisishia raia kujisajili.
Ili kutekeleza harakati hiyo kwa kiwango kikubwa, Tume ilitumia vituo 30,615 vya usajili, maafisa waliofunzwa 12,520, na vifaa vya KIEMS 5,390.
Miundombinu hii iliwezesha IEBC kudumisha viwango vya juu vya usajili kila siku, na takwimu za kila juma zilizidi wapigakura 500,000.
Mwenyekiti wa IEBC, Erastus Ethekon alisema matokeo hayo yanaonyesha azma kubwa ya umma na kuongezeka kwa imani katika mchakato wa uchaguzi.
“Shughuli hii inaonyesha nia kubwa ya kitaifa kushiriki katika mchakato wa kidemokrasia na kuashiria kiwango cha juu cha maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2027,” alisema.
Usajili wa 2026 unaonyesha mafanikio makubwa ikilinganishwa na juhudi za awali.
Mwaka 2016, awamu ya kwanza ya usajili wa wapigakura ilinasa wapiga kura milioni 1.45 katika kipindi sawa, na mnamo 2021 ilinasa karibu milioni 1.5.
Takwimu za sasa ni karibu mara mbili za matokeo hayo, ikionyesha ufanisi na utekelezaji bora.
Bw Ethekon alihusisha mafanikio hayo na mageuzi muhimu ya kiutendaji, ikiwemo mtindo rahisi zaidi wa usajili.
“Mtindo wa usajili ulioimarishwa unaokamilika umethibitika kuwa mfumo mzuri zaidi, unaojumuisha wote, wenye ufanisi na unaoweza kupanuliwa kitaifa,” alibainisha.
Shughuli hiyo pia ilijumuisha vyuo vikuu, taasisi za ufundi, na Vituo vya Huduma, kwa hivyo Tume iliwafikia vijana na wapigakura wa mara ya kwanza, ambao walikuwa sehemu kubwa ya waliojisajili.
Vijana pia walikuwa mstari wa mbele kuendesha kampeni kupitia kauli-mbiu ya Niko Kadi.
Kwa kutumia mifumo ya data ya vitambulisho na ufuatiliaji wa moja kwa moja, Tume iliweza kutambua maeneo yenye uwezekano mkubwa wa kunasa wengi kujisajili, kugawa rasilimali kwa ufanisi, na kukabiliana haraka na changamoto zilizojitokeza.
Licha ya mafanikio haya, shughuli hii ilikumbwa na changamoto kadhaa.
Tofauti za kikanda ziliendelea, hasa katika maeneo kame na yenye kiangazi ambapo matatizo ya miundombinu, umbali mkubwa, na vikwazo vya kijamii na kiuchumi vilipunguza idadi ya waliojitokeza.
Data za kaunti zinaonyesha Kaunti ya Nairobi ilirekodi idadi kubwa ya wapigakura wapya ikiwa na 276,886, ikifuatiwa na Kiambu kwa 128,859 na Nakuru kwa 102,207.
Kaunti nyingine kama Kakamega, Bungoma, na Machakos pia zilisajili idadi kubwa.
Bw Ethekon alisema tume hiyo sasa itazingatia kusafisha, kuthibitisha, na kukagua sajili ya wapigakura ili kuhakikisha usahihi na uadilifu wake.
“Mafanikio yaliyopatikana yanatoa msingi imara wa kuimarisha uadilifu na ushirikishaji wa sajili ya wapigakura ili kuwa na uchaguzi huru na wa kuaminika,” Bw Ethekon alisema.