Kesi ya Matonya kuhusu ubakaji yaanza kujikokota
AFISI ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (ODPP) bado haijamkabidhi msanii wa Bongo Flava kutoka Tanzania, Sefu Shabani Ramadhan almaarufu Matonya, stakabadhi muhimu za ushahidi zinazohusiana na kesi ya ubakaji inayomkabili.
Mahakama iliambiwa jana kuwa upande wa mashtaka haujajitayarisha kikamilifu na kwa sasa hauna vielelezo vinavyomhusisha msanii huyo na tuhuma zinazomkabili.
Aidha, mahakama ilifahamishwa hakimu aliyekuwa akisimamia kesi hiyo awali amepandishwa cheo kuwa Jaji wa Mahakama Kuu.
Upande wa mashtaka uliiomba mahakama kutoa mwelekeo zaidi kuhusu hatua zinazofuata kabla hawajapata stakabadhi muhimu.
Stakabadhi hizo zinajumuisha maelezo ya mashahidi, ripoti za matibabu zinazothibitisha madai ya ubakaji pamoja na ushahidi wa kisayansi unaoweza kumhusisha Matonya na tukio hilo.
Matonya alitiwa kizimbani kwa madai ya kutekeleza kitendo hicho cha unyama kwenye mjengo mmoja mtaani Nyali.
Ni mashtaka aliyokana msanii huy wa Bongo na akapewa dhamana ambayo amekuwa akisakasaka kuipata ili aweze kufanya kesi hiyo akiwa nje.
Alinyimwa chaguo la kutoa pesa taslimu baada ya upande wa mashtaka kuambia Mahakama kuwa si Mkenya, hivyo basi si salama kumwachilia kwa pesa taslimu.
Kama sehemu ya masharti hayo, alitakiwa kuwasilisha pasipoti yake mahakamani.
Hata hivyo, Matonya kwa sasa yuko huru baada ya kuwasilisha stakabadhi zilizohitajika na mahakama ili kuondoka gerezani alikokuwa amezuia.
Kesi hiyo imepangwa kusikilizwa Juni 17.