Siku Ruto alimjulia hali Gachagua kupitia daktari wake kipindi akivuliwa unaibu rais
RAIS William Ruto alipiga simu kwa daktari mtaalamu wa moyo aliyekuwa akimhudumia aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua siku aliyolazwa hospitalini, stakabadhi mpya za korti zimefichua, zikimvuta Rais katika matukio ya siku ya kuondolewa madarakani kwa Gachagua.
Kwa mujibu wa hati ya kiapo iliyowasilishwa mahakamani, daktari wa moyo Daniel Gikonyo alisema alipokea simu kutoka kwa Rais mnamo Oktoba 17, 2024 alipokuwa akimhudumia Gachagua katika Karen Hospital.
“Nilipokuwa nikimhudumia mlalamishi wa kwanza, nilipokea simu kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Kenya ambaye aliuliza kuhusu hali yake,” alisema Dkt Gikonyo katika kiapo chake.
Alimthibitishia Rais kuwa Gachagua alikuwa amelazwa hospitalini na alikuwa akipokea matibabu chini ya uangalizi wake.
Ufichuzi huo ni sehemu ya ushahidi katika kesi ya kikatiba inayopinga uhalali wa kuondolewa madarakani kwa Gachagua, na unaongeza uzito mpya katika mjadala wa iwapo mchakato huo ulizingatia haki na Katiba.
Dkt Gikonyo, ambaye pia ni mwanzilishi wa hospitali hiyo, aliambia mahakama kuwa amekuwa akimtibu Gachagua tangu 2006.
Alisema Gachagua, aliyekuwa na umri wa miaka 59 wakati huo, alifika hospitalini majira ya saa tisa alasiri akilalamikia maumivu makali ya kifua.
Kulingana na daktari huyo, dalili hizo zinaendana na hatari ya matatizo ya moyo, hasa kwa watu walio na umri zaidi ya miaka 45 au wenye matatizo kama shinikizo la damu, kisukari, msongo wa mawazo au unene kupita kiasi.
Alisema alimfanyia uchunguzi wa kina uliojumuisha vipimo vya damu na kipimo cha moyo (ECG) ili kubaini chanzo cha tatizo.
“Nilifanya tathmini ya kina ya kiafya ikiwemo uchunguzi wa mwili na vipimo mbalimbali vya kitabibu,” alisema.
Baada ya tathmini hiyo, alipendekeza Gachagua alazwe hospitalini kwa kati ya saa 48 na 72 ili kufuatiliwa kwa karibu na kuendelea kupokea matibabu.
Rekodi za hospitali zilizowasilishwa mahakamani zinaonyesha kuwa Gachagua alitibiwa kutokana na maumivu makali ya kifua yaliyoanza ghafla, na hali yake ilidhibitiwa kabla ya kuruhusiwa kuondoka Oktoba 20, 2024.
Ripoti ya kuondoka hospitalini inaonyesha kuwa alipewa dawa na kushauriwa kuendelea na matibabu na uchunguzi wa mara kwa mara.
Dkt Gikonyo alieleza kuwa aliwasilisha kiapo hicho ili kuthibitisha kuwa Gachagua alikuwa amelazwa hospitalini na alikuwa chini ya matibabu siku ambayo Seneti iliendelea na mchakato wa kumuondoa madarakani.
Kesi hiyo inajumuisha jumla ya maombi saba yaliyowasilishwa na walalamishi 41 akiwemo Gachagua, wanaodai kuwa mchakato wa kumuondoa madarakani ulikiuka haki yake ya kusikilizwa kwa haki.
Siku hiyo hiyo ya kulazwa kwake, Seneti iliendelea na mijadala na baadaye kuidhinisha baadhi ya mashtaka dhidi yake, hatua iliyosababisha kuondolewa kwake madarakani.
Walalamishi wanadai kuwa mchakato huo uliharakishwa na ulifanyika bila yeye kuwepo, hivyo kumnyima nafasi ya kujitetea binafsi.
Mzozo huo wa kisheria ulianza Oktoba 2024 baada ya Bunge la Kitaifa kuidhinisha hoja ya kumng’oa madarakani Gachagua kufuatia kuungwa mkono kwa mashtaka 11 yaliyowasilishwa na Mbunge wa Kibwezi Magharibi Mwengi Mutuse.
Mashtaka hayo yalijumuisha utovu mkubwa wa nidhamu, matumizi mabaya ya afisi na ukiukaji wa Katiba, ikiwa ni pamoja na madai ya kuhujumu uwajibikaji wa pamoja serikalini na kuendesha siasa za mgawanyiko.
Baada ya kura hiyo, Seneti ilifanya kikao maalumu chini ya Ibara ya 145 ya Katiba na kuidhinisha mashtaka matano, hatua iliyomng’oa rasmi madarakani siku hiyo hiyo aliyolazwa hospitalini.
Baadaye, Rais Ruto alimteua Kithure Kindiki, aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani, kuwa Naibu Rais, uamuzi ambao pia unapingwa mahakamani.
Kesi hiyo imehusisha taasisi mbalimbali za serikali zikiwemo Bunge, Mwanasheria Mkuu, Tume ya Uchaguzi na Maspika wa mabunge yote mawili, huku Rais Ruto akiwa mmoja wa washtakiwa 16.
Ushahidi wa Dkt Gikonyo sasa umeleta mwelekeo mpya katika kesi hiyo kwa kuthibitisha kuwa Gachagua alikuwa mgonjwa na kulazwa hospitalini wakati wa kura katika Seneti.
Kwa kuthibitisha kulazwa kwake pamoja na mawasiliano ya Rais, ushahidi huo unaongeza uzito katika hoja kuwa mazingira ya kuondolewa kwake madarakani yanahitaji kuchunguzwa kwa kina zaidi kisheria.
Jopo la majaji watatu linatarajiwa kupima ushahidi huo pamoja na hoja za pande zote kabla ya kutoa uamuzi kuhusu iwapo mchakato huo ulizingatia matakwa ya Katiba, ikiwemo haki ya kusikilizwa kwa haki.
Kesi hiyo inaendeleac leo.