Habari

Walimu watoa notisi ya kugoma kusimamia mitihani mwaka huu

Na LYNETTE IGADWAH July 6th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WALIMU waliokuwa wasimamizi, wasahihishaji na waangalizi wa mitihani ya kitaifa mwaka jana wameonya kuwa huenda wakasusia shughuli za mitihani ya mwaka huu ikiwa serikali haitawalipa marupurupu yao ambayo yamecheleweshwa kwa zaidi ya miezi minane.

Hatua hiyo inatishia maandalizi ya mitihani ya kitaifa ya 2026 huku vyama vya walimu vikisema vitawashauri wanachama wao kutohudhuria mafunzo ya Baraza la Mitihani la Kenya (KNEC) wala kusimamia na kusahihisha mitihani hadi watakapolipwa.

Katika hotuba ya bajeti ya mwaka wa kifedha 2026/2027 iliyosomwa Juni 11, Waziri wa Fedha John Mbadi aliwahakikishia wabunge kuwa Sh1.5 bilioni zinazodaiwa na walimu wanaosimamia mitihani zingelipwa kabla ya Juni 30, mwisho wa mwaka wa fedha 2025/2026.

Hata hivyo, tarehe hiyo ilipita bila walimu kulipwa. Afisa mmoja wa KNEC alisema baraza hilo haliwezi kulipa fedha ambazo halilipwa na Wizara ya Fedha.

Kucheleweshwa kwa malipo hayo kumeathiri maelfu ya walimu waliosimamia mtihani wa KCSE, Tathmini ya Elimu ya Msingi (KPSEA) na Tathmini ya Shule za Sekondari za Awali (KJSEA) mwaka 2025.

Kulingana na stakabadhi za bajeti, KNEC ilihitaji Sh12.7 bilioni kuendesha mitihani hiyo lakini ilitengewa Sh5.9 bilioni pekee katika bajeti ya awali.

Zaidi ya Sh1 bilioni zilitumika kulipa madeni ya mwaka uliotangulia, hali iliyoacha pengo kubwa la fedha.

Ingawa baadaye wizara ilitoa Sh3.1 bilioni kupitia bajeti ya ziada bado kulisalia upungufu wa takriban Sh4.76 bilioni.
Walimu wanasema ahadi za serikali hazijawasaidia.

Ogoro Miruka wa Shule ya Msingi ya Lang’ata West alisema alisimamia mitihani kwa siku 12 kwa malipo ya Sh500 kwa siku lakini hajapokea hata senti moja.

“Hadi sasa hatujalipwa licha ya ahadi nyingi kutoka serikalini. Walimu wanapaswa kufikiria kususia mitihani ya mwaka huu,” alisema.

Mwalimu mwingine ambaye hakutaka kutajwa jina alisema kucheleweshwa kwa malipo kumevunja moyo walimu wengi.

“Hapo awali tulilipwa mara tu matokeo yalipotangazwa, lakini wakati huu hakuna aliyelipwa licha ya ahadi za mara kwa mara,” alisema.

Evans Ochieng’ wa Shule ya Riruta Satellite Junior alisema hata baadhi ya wasahihishaji wa mitihani bado hawajalipwa kikamilifu.

Naibu Katibu Mkuu wa KUPPET, Moses Nthurima, alisema kucheleweshwa kwa malipo kwa miezi minane hakukubaliki.

“Serikali inapaswa kuhakikisha shughuli muhimu kama hizi zinafadhiliwa kwa wakati, la sivyo ubora wa elimu utaathirika,” alisema.

Katibu Mtendaji wa KNUT tawi la Nairobi, Mugwe Macharia, alisema walimu wamekuwa wakipiga simu ofisi za chama wakitaka hatua ichukuliwe.

“Ikiwa fedha hazitalipwa, tutawashauri wanachama wetu wasihudhurie mafunzo ya KNEC na tunazingatia pia kuwashauri wasisimamie mitihani ya mwaka huu,” alisema.