MAONI: Kalonzo ajitafutie kura la sivyo atarukwa kama 2013
KINARA Wiper Kalonzo Musyoka anastahili kutafuta kura zake kwanza kabla ya kutegemea uungwaji mkono wa viongozi wenzake kwa sababu suala la kuidhinishwa kwake huenda likagawanya upinzani kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Wiki jana kulikuwa na gumzo kuhusu kauli ya aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua kuwa hana muafaka wowote wa kuunga azma ya makamu huyo wa rais wa zamani.
Bw Gachagua ambaye amekuwa na kikao cha kuwasikiliza wanasiasa na makundi mbalimbali ya kijamii nyumbani kwake Wamunyoro, Nyeri, aliweka bayana kuwa hakuna maafikiano yoyote kati yake na Bw Musyoka kuhusu 2027 na kuwa mazungumzo bado yanaendelea.
Katika ziara aliyokuwa nayo Ukambani mnamo Machi 30 2026, Bw Gachagua alimmiminia Bw Musyoka sifa kedekede na kuashiria kuwa atakuwa nyapara wa upinzani katika kinyang’anyiro cha urais mwakani.
Katika msururu wa mikutano ya siku tano Ukambani, Bw Gachagua alimrejelea Kalonzo kama msemaji wa upinzani huku pia akisema ana uzoefu wa uongozi kumwezesha kuwa rais wa sita wa Kenya.
Zaidi ya miezi mitatu baadaye, mambo yanaonekana kubadilika huku Bw Gachagua akibadili wimbo na kauli zake nyingi zikimnukuu akisema yuko tayari kuunga mtu yeyote katika upinzani lakini baada ya mazungumzo.
Wandani wa Bw Musyoka kama vile Seneta wa Kitui, Enock Wambua nao wamekuwa wakirindima ngoma ya Bw Musyoka na kusisitiza kuwa ataungwa mkono na Mlima Kenya.
Hata hivyo, Bw Musyoka anastahili kujihadhari na kuanza kujitafutia kura badala ya kutegemea tu za Mlima Kenya.
Kuelekea uchaguzi mkuu wa 2013, Bw Musyoka alikuwa mshirika wa Uhuru Kenyatta na William Ruto na wakati wa mazungumzo ya kusaka muafaka wa uchaguzi, alipigwa kumbo kutokana na kura zake zilizoonekana kuwa chache.
Hii ndiyo hali itakayomkabili tena kwa sababu Bw Gachagua mwenyewe amewahi kumshajiisha aje mezani na kura nyingi.
Ni dharau ya kutokuwa na kura nyingi 2013 ndiyo iliyosababisha aondoke kambi ya UhuRuto na kuwa mgombeaji mwenza wa Raila Odinga.
Kwa muda sasa Bw Musyoka amekita siasa zake Ukambani na wakati mwingine Mlima Kenya.
Amekuwa akienda ziara maeneo mengine tu iwapo vinara wa upinzani wanahudhuria mikutano maeneo hayo.
Makamu huyu wa rais wa zamani anafaa kuzinduka na aanze kujitafutia kura Nyanza, Pwani, Magharibi, Bonde la Ufa na Kaskazini Mashariki badala ya kutegemea Mlima Kenya pekee.
Akumbuke kuwa mbali na DCP, Naibu Kiongozi wa Jubilee Dkt Fred Matiang’i pia analenga kura za eneo hilo 2027.
Kwa hivyo, Bw Musyoka hajahakikishiwa uungwaji kutoka Mlima Kenya kiasi cha kufananishwa na walivyompigia Rais Ruto 2022 au Uhuru na Kibaki kwenye chaguzi za nyuma.
Eneo la Ukambani lina Kaunti za Machakos, Kitui na Makueni kulingana na makadirio ya Tume ya Uchaguzi (IEBC) mnamo 2027, Machakos itakuwa na wapigakura 883, 629, Kitui kura 684,878 kisha Makueni 616,104 kufikia 2027.
Hizi ni karibu kura milioni mbili ambazo hazitoshi kumpa Bw Musyoka urais ndiposa lazima asake uungwaji mkono kwa maeneo yote badala ya mlima pekee ambayo pia hana uhakika nao.
Isitoshe wakazi wa Mlima Kenya nao wanaangalia watashikilia wadhifa upi wa juu na kauli ya kila mara ya Bw Gachagua kuwa atawania urais inastahili kumtia Bw Musyoka wasiwasi.
Ni wazi suala la Kalonzo kuwa mwaniaji wa upinzani limeibua wasiwasi na mgawanyiko miongoni mwa vinara wa upinzani.
Faraja kwake itakuwa ni kuzidisha juhudi kuwahi kura nyingi la sivyo atarukwa kama 2013. Siasa haina urafiki wa milele na hakikisho la kudumu.