Habari

Vyama vya kisiasa vyatakiwa kuzingatia sheria uchaguzi mkuu ukikaribia

Na WINNIE ONYANDO May 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MWENYEKITI wa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa nchini (ORPP), John Lorionokou, amevitaka vyama vya kisiasa kuzingatia sheria na kanuni zinazoongoza shughuli zao kuelekea uchaguzi mkuu ujao.

Akizungumza wakati wa kukabidhi cheti cha usajili kwa chama cha Kenya United Generation (KUG) katika ofisi za ORPP jijini Nairobi, Lorionokou alisema baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakitumia vyama vya kisiasa kujinufaisha badala ya kuhudumia wananchi.

Alisema ni muhimu kwa vyama vya siasa kuhakikisha vinafuata sheria zilizowekwa ili kudumisha uwajibikaji, uwazi na demokrasia nchini.

“Vyama vya kisiasa vina nafasi muhimu katika kuimarisha demokrasia. Ni lazima viongozi na wanachama waheshimu sheria na kanuni za vyama vyao,” alisema.

Lorionokou pia alisisitiza umuhimu wa vyama kuwapa vijana nafasi ya kushiriki katika uongozi na maamuzi ya kisiasa.

Kwa upande wake, kinara wa chama cha KUG, Vincent Munywoki, alisema usajili wa chama hicho ni hatua muhimu kwa vijana wanaotaka kuingia katika siasa.

Munywoki alisema vijana wengi wamekuwa wakitengwa katika nafasi za uongozi licha ya kuwa na uwezo wa kuleta mabadiliko nchini.

“Ni wakati wa vijana kusimama na kuwania nyadhifa mbalimbali za kisiasa ili kushiriki katika maendeleo ya taifa,” alisema.

Aliongeza kuwa chama chake kitajikita katika ajenda za vijana, uwajibikaji na maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Bw Lorionokou ni afisa wa zamani wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).