Habari

Waziri Ruku akumbana na uzembe wa watumishi wa umma afisi za serikali Garissa

Na MANASE OTSIALO May 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WAZIRI wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku, mnamo Alhamisi alishtushwa na hali duni ya utoaji huduma katika afisi za serikali mjini Garissa, baada ya kukuta afisi nyingi zikiwa zimefungwa na watumishi kukosekana kazini.

Waziri huyo, aliyesafiri hadi Garissa usiku wa kuamkia Alhamisi, aliwasili katika afisi za ukanda huo asubuhi, lakini akakumbana na viti vitupu na milango iliyofungwa.

Jengo linalohifadhi afisi mbalimbali za serikali lilikuwa na afisa mmoja pekee, wakati msafara wa Waziri Ruku ulipowasili.

“Nimesikitika sana asubuhi ya leo. Niko katika afisi zinazoratibu huduma zote za eneo hili lakini hakuna kinachoendelea. Afisi zote za serikali ambazo zinapaswa kufunguliwa saa moja na nusu asubuhi bado zimefungwa,” alisema.

Kwa mujibu wa Waziri Ruku, mwongozo wa wafanyakazi wa mwaka wa 2016 unaelekeza kuwa afisi zote za serikali katika eneo la Kaskazini Mashariki kufunguliwa saa moja na nusu asubuhi na kufungwa kwa mapumziko ya saa mbili wakati wa mchana kabla ya kazi kuendelea saa nane na nusu mchana hadi saa kumi na nusu jioni.

Mapumziko hayo ya saa mbili hutolewa ili kuruhusu Waislamu kutekeleza ibada za sala.

Kamishna wa Kanda ya Kaskazini Mashariki, John Otieno, ambaye hakuwepo wakati huo, aliripotiwa kuwa mjini Wajir akisimamia maandalizi ya sherehe za Madaraka Day zitakazofanyika Juni 1, 2026.

Waziri huyo alisema hakuna sababu ya watumishi wa umma kulegea katika utoaji huduma ilhali serikali imeongeza mishahara yao.

“Watumishi wote wa umma wanapaswa kuwa makini na kazi yao. Mishahara yenu iliongezwa Januari mwaka huu na ikawekwa kuanzia Julai 1, 2025,” alisema.