Gachagua alitimuliwa kuzima upinzani ndani ya serikali, mahakama yaambiwa
WALALAMISHI wanaokosoa kuondolewa madarakani kwa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua, wameambia Mahakama Kuu kuwa mchakato huo haukuwa wa kikatiba bali ulipangwa kisiasa kwa lengo la kuondoa upinzani ndani ya serikali ya Kenya Kwanza.
Wakiwakilishwa mbele ya jopo la majaji watatu wa Kitengo cha Katiba na Haki za Binadamu, na mawakili wao, walalamishi hao walisema kuondolewa kwake kulifanywa kupitia Bunge “lililotekwa na serikali kuu”, kumlinda Rais William Ruto dhidi ya upinzani ndani ya serikali yake.
Walidai kuwa mchakato mzima wa Oktoba 2024 ulitokana na mzozo wa kisiasa ndani ya serikali, na si ukiukaji wa Katiba kama ilivyodaiwa bungeni na Seneti wakati wa kumuondoa Bw Gachagua madarakani.
Kesi hiyo, ambayo sasa imeibua mjadala mkubwa wa kikatiba nchini, inaangazia kile walalamishi wanakiita “kuporomoka kwa mifumo ya uangalizi wa Katiba” kupitia matumizi ya Bunge kama chombo cha kulinda maslahi ya kisiasa.
Wakili Jane Njeri Maina, ambaye pia ni Mbunge wa Kike Kaunti ya Kirinyaga, aliambia mahakama kuwa Bunge lilikiuka maagizo ya mahakama yaliyotaka kuwepo kwa ushirikishaji wa wananchi katika ngazi ya maeneo bunge kabla ya kura ya kumuondoa Bw Gachagua kupigwa.
Alisema badala ya kufanya mikutano ya maana ya ushirikishaji wa umma, Bunge lilichapisha fomu ya “NDIO/HAPANA” kwenye gazeti la kitaifa na kukusanya takriban majibu 200,000 pekee kutoka kwa zaidi ya wananchi milioni 52.
“Utaratibu huu haukutoa nafasi ya mjadala wa kina wala ushiriki wa wananchi. Ilikuwa ni mchakato wa haraka uliolenga matokeo yaliyopangwa tayari,” alisema Bi Maina.
Aliongeza kuwa Bunge la Taifa lilipunguza mashtaka ya kikatiba dhidi ya Bw Gachagua kuwa kura rahisi ya kukubali au kukataa, jambo alilosema lilikiuka misingi ya haki ya kusikilizwa kwa haki.
Baada ya kura hiyo, Bunge lilipitisha hoja ya kumuondoa mamlakani Bw Gachagua kwa kura 281 dhidi ya 44, kisha Seneti ikaidhinisha uamuzi huo kwa kura 54 dhidi ya 13, wakati ambao alikuwa amelazwa hospitalini.
Walalamishi pia walilaumu Seneti kwa kushindwa kuunda kamati maalum ya wanachama 11 kama inavyotakiwa na Ibara ya 145 ya Katiba, wakisema badala yake Seneti iliketi kama Kamati ya Bunge Zima.
Kulingana nao, hatua hiyo ilifuta hatua muhimu ya uchunguzi na kumnyima Bw Gachagua haki ya kujitetea kikamilifu kabla ya uamuzi kufikiwa.
“Kamati maalum si mapambo ya kiutaratibu. Ni kiini cha uchunguzi wa kuondolewa mamlakani. Bila kamati hiyo, mchakato haukufuata Katiba,” alisema Bi Maina.
Wakili Kibe Mungai, anayewakilisha kundi lingine la walalamishi kikiwemo chama cha mawakili wa Mlima Kenya Gema Watho Association, alisema mchakato huo ulikuwa sehemu ya mpango wa kisiasa wa mapema kuelekea uchaguzi wa 2027.
Alidai kuwa tofauti za kisiasa ndani ya Kenya Kwanza, hasa kuhusu maandamano ya Gen Z na masuala ya ugavi wa madaraka, zilichochea hatua hiyo ya kumuondoa Bw Gachagua mamlakani.
“Bunge lilitumika kama silaha ya kisiasa. Huu haukuwa mchakato wa kikatiba bali wa kuondoa mpinzani wa kisiasa ndani ya serikali,” alisema Bw Mungai.
Walalamishi walidai kuwa Bunge na Seneti ziliacha uhuru wao wa kikatiba na kugeuka kuwa sehemu ya Ikulu.
Walisisitiza kuwa iwapo Bunge linaweza kutumika kumuondoa Naibu Rais bila kufuata Katiba kikamilifu, basi hakuna afisi ya kikatiba iliyo salama nchini.
Wakili Ndegwa Njiru alisema mchakato huo ulikuwa “dhihaka ya Katiba”, akidai Bw Gachagua alinyimwa haki ya msingi ya kusikilizwa kwa haki chini ya Ibara ya 50.
Walalamishi sasa wanaomba mahakama kufuta maamuzi ya Bunge na Seneti, pamoja na kubatilisha uteuzi wa Profesa Kithure Kindiki kama Naibu Rais.
Kesi hiyo inaendelea kusikilizwa huku ikitarajiwa kuathiri kwa kina tafsiri ya Katiba kuhusu mchakato wa kumuondoa Naibu Rais nchini Kenya.