SHA: Kesi yawasilishwa kupinga mfumo wa ufadhili wa afya nchini
MFUMO mpya wa ufadhili wa huduma za afya nchini, ukiwemo Mamlaka ya Afya ya Kijamii (SHA), umepata pigo baada ya mwanaharakati Francis Awino kuwasilisha kesi katika Mahakama Kuu ya Kiambu akipinga uhalali wake kisheria.
Katika kesi hiyo, Awino anahoji kuwa baadhi ya shughuli chini ya mfumo huo wa afya zinafanywa bila kufuata sheria na kuzingatia uwazi.
Miongoni mwa shughuli hizo ni makato ya michango, uchakataji wa madai ya matibabu na usimamizi wa mafao ya wanachama.
Waliojumuishwa katika kesi hiyo ni Wizara ya Afya, Hazina ya Kitaifa, SHA, Mamlaka ya Afya ya Kidijitali, Tume ya Utumishi wa Umma (PSC) na Tume ya Huduma kwa Walimu (TSC).
Awino anadai kuwa shughuli hizo ni kama kufanya biashara ya bima, hivyo zinapaswa kufanywa tu ikiwa kuna sheria inayoidhinisha wazi taasisi husika kufanya kazi hiyo.
Aidha, anahoji uhalali na uthabiti wa mfumo wa Hazina ya Bima ya Afya ya Kijamii akisema utekelezaji wake unaibua maswali ya kikatiba na kisheria.
Kupitia kwa kesi hiyo, mwanaharakati huyo anaomba mahakama kutoa amri za kusimamisha kwa muda utekelezaji na upanuzi wa mfumo huo hadi kesi itakaposikizwa na kuamuliwa.
Pia anaomba mahakama itangaze kuwa SHA na taasisi nyingine za umma haziwezi kuendesha shughuli za bima, au kushughulikia madai ya matibabu bila idhini ya moja kwa moja ya sheria.
Jaji Bahati Mwamuye ameagiza wahusika wote kuwasilisha stakabadhi za kesi kufikia Mei 8, 2026 huku majibu yao yakitarajiwa kuwasilishwa kabla ya Mei 22, 2026.
Kesi hiyo itatajwa tena Juni 9, 2026 kwa maelekezo zaidi.