HabariHabari za Kitaifa

Kongamano la bara Afrika laonyesha ubunifu wa sanaa Kenya

Na SAMMY WAWERU May 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KONGAMANO la mwaka huu, 2026, kuonyesha bunifu za kisanaa lililoandaliwa na muungano wa wanawake kwenye teknolojia na bunifu barani Afrika limefanyika jijini Nairobi, likiiweka Kenya kwenye ramani ya kimataifa kuhusu bunifu na vumbuzi zake kisanaa na kidijitali.

Hafla ya muungano huo, kwa Kiingereza Women in Technology and Innovation Africa, ilifanyika katika Mkahawa wa Safari Park, jijini Nairobi Ijumaa, Mei 8, ikileta pamoja wanasanaa, wabunifu, wanafunzi, wajasiriamali, washirika wa maendeleo na taasisi mbalimbali kutoka kote nchini.

Kongamano hilo linalojulikana kama WITIA Creative Show Makala ya 2026, pia lilileta pamoja wasanii, wavumbuzi, watunga sera na wadauhusika masuala ya utamaduni, likilenga kuangazia uhusiano unaozidi kukua kati ya sanaa, teknolojia na ubunifu, ili kusaidia kuboresha uchumi wa Kenya.

Aidha, hafla hiyo iliandaa jukwaa la maonyesho ya kitamaduni, bidhaa za sanaa na kazi za ubunifu, mafunzo ya kubuni mitandao, ikiwa ni pamoja na kugaragaza mijadala kufanikisha bunifu za kiteknolojia na kidijitali barani Afrika.

Akizungumza wakati wa kongamano hilo, Katibu katika Idara ya Uchumi wa Ubunifu, Fikirini Jacobs, alipigia upatu utandawazi wa ubunifu nchini Kenya akisema una uwezo mkubwa kuzalisha ajira haswa kwa vijana na kuleta mageuzi kimaendeleo.

“Majukwaa kama ya WITIA Creative Show yanaonyesha jinsi teknolojia, utamaduni na ubunifu, vyote vinaweza kushirikiana kuunda nafasi endelevu kwa vijana na wajasiriamali wa sekta ya ubunifu,” alisema. Kulingana na Bw Fikirini, sekta hiyo inaweza kusaidia kukuza ubunifu, biashara na maendeleo ya taifa iwapo vipaji vitaungwa mkono ipasavyo.

Picha ya juu kuonyesha wajumbe walioshiriki Kongamano la Women in Technology and Innovation Africa (WITIA) Creative Show Makala ya 2026 mnamo Ijumaa, Mei 8 Safari Park Hotel, Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Naye Katibu katika Idara ya Biashara Ndogo Ndogo na za Wastani (MSMEs), Susan Mang’eni, alielezea kwamba biashara zenye nyenzo za ubunifu zinaendelea kuwa nguzo muhimu kwa wafanyabiashara nchini – haswa wenye mapato ya chini.

“Kuunga mkono wasanii, wavumbuzi na wajasiriamali wa kitamaduni kupitia sera, upatikanaji wa masoko na ushirikiano ni muhimu katika kuimarisha maisha ya wananchi na kupanua ushirikishwaji wa kiuchumi,” Bi Mang’eni alisema. Katibu huyo alielezea jinsi serikali imejitolea kuunda mifumo ya kutambua vipaji, kutoa mafunzo na ushauri nasaha kwa vijana wenye uwezo katika sekta ya ubunifu.

Kauli ya Bi Mang’eni ilitiliwa mkazo na Peter Karanja – Mkurugenzi Msaidizi, Idara ya Masuala ya Vijana, aliyesema serikali tayari imeanzisha majaribio ya mpango wa Talent Search Program katika Kaunti ya Kwale, ukilenga vipaji vya muziki, densi, mitindo, vichekesho, mashairi, mashindano ya urembo na utengenezaji majukwaa ya kidijitali. “Mpango huu sio mashindano pekee, bali pia ni jukwaa la mafunzo, ushauri, usaidizi wa bidhaa, nafasi za soko na biashara,” alisema.

Changamoto kwenye sekta ya ubunifu  

Afisa huyo alieleza kuwa licha ya Kenya kuwa na vipaji vingi, wabunifu wengi bado hawana mifumo madhubuti ya kukuza na kudumisha kazi zao.

Aidha, alisikitika kwamba wanawake bado hawajawakilishwa ipasavyo katika sekta nyingi za teknolojia na ubunifu licha ya mchango wao mkubwa katika uchumi. “Serikali imejitolea kuhakikisha kina mama na wasichana wanapata nafasi, ujuzi, uongozi, ufadhili na majukwaa ya kidijitali.”

Alitaja changamoto zingine zinazokumba sekta ya ubunifu kama ukosefu wa ufadhili wa kutosha, mifumo dhaifu ya biashara, miundombinu duni ya ubunifu, changamoto za hakimiliki na ukosefu wa usawa wa kidijitali.

Baadhi ya wanawake wajumbe walioshiriki Kongamano la Women in Technology and Innovation Africa (WITIA) Creative Show Makala ya 2026 mnamo Ijumaa, Mei 8 Safari Park Hotel, Nairobi. Picha|Sammy Waweru

Eunice Pohlmann, mwanzilishi wa WITIA, alisema maonyesho hayo yaliandaliwa kwa lengo kuunganisha sanaa, teknolojia na ubunifu ili kufungua nafasi mpya kwa wabunifu barani Afrika.

“WITIA Creative Show inapiku hafla; ni shughuli inayolenga kuunganisha sanaa, teknolojia na ubunifu,” alisema. Aliongeza kuwa mustakabali wa Afrika uko mikononi mwa wabunifu wanaoweza kuunganisha utamaduni, simulizi na zana za kidijitali.

Kwa upande wake, Dkt Bella Namango, mwanachama mshauri wa WITIA, alisema mwingiliano kati ya teknolojia na sanaa unabadilisha jinsi jamii zinavyohifadhi urithi wa kitamaduni na kuwasilisha mawazo.

“Kwa kuleta pamoja wabunifu na wavumbuzi, tunafungua mianya ya ushirikiano, utafiti, elimu na ukuaji endelevu ndani ya uchumi wa ubunifu,” alisema.

Maonyesho hayo, pia, yalitumika kuonyesha vipaji katika kuburudisha na vipindi vya kujenga mitandao vitakavyoleta pamoja wabunifu, wawekezaji, taasisi za elimu na watunga sera ili kuimarisha ushirikiano katika sekta ya ubunifu nchini Kenya.