Habari

Mwanasheria Mkuu atetea uteuzi wa Kindiki kuwa Naibu Rais baada ya Gachagua kutimuliwa

Na JOSEPH WANGUI May 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MWANASHERIA Mkuu, Dorcas Oduor, amesihi Mahakama Kuu kutobatilisha kuondolewa mamlakani kwa Bw Rigathi Gachagua kama Naibu Rais, akisema majaji hawana mamlaka ya kupitia upya maamuzi ya kisiasa yaliyofanywa na Bunge.
Kupitia wakili wake, Profesa Githu Muigai, Mwanasheria Mkuu pia alitetea uteuzi wa Profesa Kithure Kindiki kuchukua nafasi ya Bw Gachagua baada ya kuondolewa kwake Oktoba 2024, akisema hatua hiyo ilikuwa mamlaka ya kipekee ya Rais William Ruto chini ya Katiba na haikuhitaji idhini ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC).
Kauli hiyo ilikuwa jibu kwa walalamishi waliodai kuwa uteuzi wa Prof Kindiki ulikuwa batili kwa sababu ulifanywa wakati ambao IEBC haikuwa na makamishna wa kuthibitisha ufaafu wake.
Prof Muigai alisema mchakato wa kumteua Naibu Rais mpya unahusisha wahusika wawili pekee ambao ni Rais anayemteua na Bunge la Kitaifa linaloidhinisha au kukataa uteuzi huo.
“Rais anateua na Bunge linaweza kukubali au kukataa. Hao ndio wahusika pekee,” alisema mbele ya jopo la majaji watatu wanaosikiliza kesi zilizounganishwa kupinga kuondolewa kwa Bw Gachagua mamlakani.
Aliongeza kuwa kushirikisha IEBC kungekuwa tu hatua ya hiari ya uhakiki na si hitaji la kikatiba.
Prof Muigai alisema jukumu la mahakama ni kuamua iwapo haki za kikatiba za Bw Gachagua zilikiukwa wakati wa mchakato wa kumtimua, na si kupitia upya ushahidi au maamuzi ya Bunge.
 “Mahakama haiwezi kubadilika kuwa chombo cha kukata rufaa dhidi ya maamuzi ya kisiasa ya Bunge,” alisema.
Wakati huo huo, mawakili wa Bunge la Kitaifa na Prof Kindiki walitangaza nia ya kumhoji daktari mtaalamu wa moyo, Dkt Daniel Gikonyo, kuhusu hati yake ya kiapo inayodai Bw Gachagua alikuwa amelazwa hospitalini wakati ambao Seneti ilikuwa ikijadili hoja ya kumng’atua mamlakani.
Katika hati hiyo, Dkt Gikonyo alisema Rais Ruto alimpigia simu Oktoba 17, 2024 kuulizia hali ya Bw Gachagua aliyekuwa amelazwa katika Hospitali ya Karen akilalamikia maumivu makali ya kifua.
Mawakili wa washtakiwa katika kesi hiyo walipinga hati hiyo wakisema iliwasilishwa kuchelewa na ilileta ushahidi mpya baada ya kesi kuendelea kwa kiwango kikubwa.
Hata hivyo, mahakama ilikubali hati hiyo “kwa maslahi mapana ya haki”.
Prof Muigai alisisitiza kuondolewa mamlaka ni mchakato wa kisiasa uliowekwa mikononi mwa wabunge na maseneta, si majaji.
Alisema Katiba iliweka viwango vya juu kuhakikisha kuwa uamuzi huo unabaki kuwa mamlaka ya Bunge.
“Usiku ambao Seneti ilipiga kura, mlalamishi alikuwa tayari ameondolewa mamlakani. Hakukuwa na haja ya hatua nyingine yoyote,” alisema.
Kesi hiyo itaendelea Mei 13 huku mahakama ikitarajiwa kusikiliza hoja zaidi za pande zote.