Habari

Magavana wataka walipwe pensheni baada ya kustaafu

Na VITALIS KIMUTAI May 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

HARAMBEE iliyopangwa kusaidia matibabu maalum ya aliyekuwa Gavana wa Kericho Profesa Paul Chepkwony imefichua maisha magumu wanayokumbana nayo baadhi ya magavana baada ya kuondoka afisini kutokana na ukosefu wa mpango wa pensheni na bima ya afya.
Licha ya hadhi kubwa wanayokuwa nayo wakikuwa mamlakani, wakiwa na misafara ya magari, walinzi, wasaidizi na kuitwa “Waheshimiwa”, baadhi ya magavana waliostaafu ambao hawakuwa na misingi imara ya kifedha wamerejea maisha ya kawaida.
Profesa Chepkwony, aliyekuwa gavana kwa mihula miwili, amekuwa akiugua kwa miaka mitano iliyopita na ameishi maisha ya faragha huku akilazwa hospitalini mara kwa mara.
Mmoja wa jamaa zake alisema familia pamoja na viongozi wa Kericho wanapanga mchango katika Hoteli ya Weston jijini Nairobi kufadhili matibabu yake nje ya nchi.
Masaibu ya gavana huyo wa zamani sasa yameibua mjadala kuhusu hali halisi ya maisha ya viongozi baada ya kuondoka mamlakani.
Kwa sasa, magavana hupokea marupurupu ya asilimia 31 kila mwaka waliotumikia lakini hawana pensheni wala bima ya afya baada ya mihula yao ofisini.
Pia hupoteza walinzi, wapishi, madereva, watunza bustani na wafanyakazi wengine wa nyumbani waliokuwa wakigharamiwa na serikali wakiwa afisini.
Hali hiyo imezua maswali kuhusu iwapo ukosefu wa mpango wa pensheni ni moja ya sababu zinazochangia ufisadi katika serikali za kaunti.
Wabunge wanaohudumu kwa mihula miwili hupokea pensheni ya maisha, lakini magavana na manaibu wao hawafaidiki na mpango kama huo licha ya kushikilia nyadhifa kubwa katika serikali za kaunti.
Kwa mujibu wa Tume ya Mishahara na Marupurupu (SRC), gavana hupokea mshahara wa jumla wa Sh900,000 kwa mwezi huku naibu gavana akipokea Sh684,233.
Mbali na mishahara hiyo, viongozi hao hupata magari rasmi, mikopo ya magari na nyumba pamoja na bima ya afya kwa familia zao wanapokuwa afisini.
Gavana na naibu wake pia hupata bima ya matibabu inayojumuisha Sh10 milioni za matibabu ya kulazwa hospitalini, Sh300,000 kwa matibabu ya nje, Sh150,000 za uzazi na Sh75,000 kwa huduma za meno na macho.
Lakini manufaa hayo yote hukoma wanapoondoka mamlakani wanaposhindwa kwenye uchaguzi, kuondolewa afisini au kumaliza mihula yao miwili.
Mnamo Januari 2026, Rais William Ruto aliongoza chama cha UDA kuunga mkono kuanzishwa kwa mpango wa pensheni kwa magavana, manaibu wao, maspika wa mabunge ya kaunti na madiwani.
“Lazima tuhakikishe viongozi waliotumikia wananchi hawageuki kuwa fedheha kwa jamii baada ya kuondoka mamlakani,” alisema Rais Ruto.
Rais alisema serikali itahakikisha mpango huo umejumuishwa katika bajeti ya mwaka wa kifedha wa 2026/2027.
Mwenyekiti wa Baraza la Magavana Ahmed Abdullahi alisema viongozi wa kaunti wamejitolea sana kwa maendeleo ya jamii na wanastahili kulindwa kupitia mpango wa pensheni.
“Kiongozi wa kaunti hujitolea kwa maendeleo ya wananchi wake na ni muhimu awe na maisha ya heshima baada ya kuondoka afisini,” alisema.

Kiongozi wa wengi katika seneti Aaron Cheruiyot na Kiongozi wa Wengi katika Bunge la Kitaifa Kimani Ichung’wah pia wameunga mkono pendekezo hilo wakisema litawalinda viongozi dhidi ya umaskini baada ya kuondoka afisini.
Wakili wa Nairobi Kipkirui Kap Telwa alisema ukosefu wa pensheni una uhusiano mkubwa na ongezeko la ufisadi katika serikali za kaunti.
 “Huwezi kumpa mtu usimamizi wa mabilioni ya fedha kila mwaka halafu umwambie baada ya kuondoka afisini hatakuwa na hata bima ya afya. Hilo linaweza kuwafanya baadhi yao kuiba ili kujihakikishia maisha ya baadaye,” alisema.
Hata hivyo, Mahakama Kuu mnamo Julai 2024 iliamua kuwa magavana na manaibu wao hawastahili mpango wa pensheni wa viongozi wa serikali kuu kwa sababu si endelevu kiuchumi.
Katika kesi hiyo iliyowasilishwa na Baraza la Magavana dhidi ya SRC, Jaji Lawrence. Mugambi alisema mpango huo ungekuwa mzigo mkubwa kwa aifa.
Pendekezo la mwaka 2021 la kuanzisha mpango wa pensheni kwa viongozi wa kaunti lilipendekeza gavana aliyehudumu mihula miwili alipwe Sh11.1 milioni kama mkupuo na pensheni ya Sh739,200 kila mwezi maisha yake yote.
Sasa macho yote yanaelekezwa kwenye bajeti ijayo kuona iwapo serikali itatekeleza ahadi ya kuanzisha mpango huo wa pensheni kwa viongozi wa kaunti.