Tshisekedi adokeza kuwania urais kwa muhula wa tatu
RAIS wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Félix Tshisekedi amedokeza uwezekano wa kuwania muhula wa tatu huku akisema huenda uchaguzi ukachelewa hadi 2028 kutokana na vita vinavyeondelea mashariki.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari mjini Kinshasa, Tshisekedi alisema iwapo watu watamtaka awe kwenye kingang’anyiro, basi hatakuwa na budi ila kutii matakwa yao.
“Mimi sijataka kuwania tena ila watu wakitaka niwe pale tena, mimi ni nani, nitatii tu,” akasema rais huyo.
Kulingana na katiba ya sasa ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, mtu anaweza kuiongoza nchi hiyo kwa mihula miwili pekee.
Hii ina maana kuwa huenda katiba ikabadilishwa iwapo atakuwa kwenye kinyang’anyiro.
Upinzani ndani ya taifa hilo umekuwa ukimtuhumu Tshisekedi kuwa na nia ya kuibadilisha katiba ili aendelee kutawala, ukisema hatua yoyote katika mwelekeo huo utakuwa mapinduzi ya katiba.
Serikali ya Congo imekuwa ikipambana na waasi wa M23, ambao inaaminika sana kuungwa mkono na nchi jirani ya Rwanda, pamoja na vikundi vingine vya wenyeji vilivyoko Mashariki mwa Congo kwa miaka kadhaa.
Rwanda hata hivyo, imekuwa ikikanusha madai ya kuwaunga mkono waasi hao.
Kutokana na hilo, Amerika iliwaadhibu baadhi ya makamanda wa jeshi la Rwanda Machi, ikiwashutumu kwa kuchochea mzozo wa Congo, huku mapigano yakiendelea licha ya makubaliano ya amani yaliyosimamiwa na Washington.
Tshisekedi hata hivyo, amekuwa akisisitiza kwamba, kipaumbele chake kilikuwa kurejesha amani kupitia diplomasia kabla ya kuondoka madarakani.