Habari

Mauaji ya akina mama yazidi nchini huku tukiadhimisha Siku ya Akina Mama duniani

Na WAANDISHI WETU  May 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

VISA vya mauaji ya wanawake na wasichana nchini Kenya vinaendelea kushtua taifa, kila kisa kikiwa na maumivu mapya na maswali mazito kuhusu usalama wa wanawake katika jamii.
Kutoka mashambani hadi mijini, kutoka Pwani hadi Bonde la Ufa, visa hivi vinaonyesha mtindo unaozidi kuongezeka wa ukatili unaohusishwa na mapenzi yaliyovunjika, migogoro ya kifamilia na hasira zisizodhibitiwa.
Katika Kaunti ya Bomet, Ivine Cheche Chepkoech, msichana wa miaka 17, aliuawa kikatili akiwa nyumbani kwa nyanya yake.
Alikuwa akiandaa chakula cha jioni kabla ya kushambuliwa kwa kitu kizito kichwani na baadaye kukatwa kwa kitu chenye ncha kali. Mwili wake baadaye ulipatikana ukiwa umetupwa katika shamba la chai.
Polisi wanamshuku mpenzi wake wa zamani kuwa mhusika wa shambulio hilo.
Katika Kaunti ya Nakuru, mauaji ya wanawake yamechukua sura ya kutisha zaidi.
Mwanamke mmoja, Annita Mugweru, aliuawa kwa kudungwa kisu akiwa nyumbani kwake kufuatia mzozo wa kifamilia, tukio lililotokea mbele ya mtoto wake mdogo.
Katika tukio jingine, mlinzi, Jackline Awuor, alipatikana ameuawa na kichwa kukatwa katika eneo la Bahati, baada ya kutoweka kazini, huku mpenzi wake akihusishwa na mauaji hayo.
Huko Siaya, kijana wa miaka 21, Rose Benta Apondi, alipatikana akiwa ameuawa baada ya kutoweka kwa wiki mbili. Familia yake ilieleza kuwa alikuwa akipokea vitisho kutoka kwa mpenzi wake wa zamani baada ya kuvunja uhusiano. Mwili wake ulikuwa umeharibika vibaya kiasi cha kufanya uchunguzi wa kifo kuwa mgumu.
Katika eneo la Meru, mwanafunzi Diana Cherono, miaka 20, alipatikana ameuawa na mwili wake kutupwa kwenye bomba la maji taka wiki kadhaa baada ya familia yake kumtafuta bila mafanikio. Tukio hilo liliwaacha wazazi wake wakiwa na majonzi makubwa baada ya kugundua kuwa binti yao alikuwa tayari ameuawa mbali na nyumbani.
Katika Bonde la Ufa, mkasa mwingine uliogusa hisia ni wa familia ya Elgeyo Marakwet, ambapo mwanamume alimuua mke wake na watoto wake wawili kutokana na mgogoro wa kifamilia. Katika kaunti ya Baringo, mwanamume mwingine alimuua mkunga akimlaumu kwa kifo cha mtoto wake mchanga. Mshukiwa alitumia mshale wenye sumu.
Pwani nayo haijaachwa nyuma. Katika kaunti za Mombasa na Kilifi, visa vya wanawake na watoto kuuawa kikatili vimeongezeka. Mwanamke mjamzito alipatikana ameuawa na mwili wake kutupwa ndani ya jengo ambalo halijakamilika. Mtoto wa miaka minane naye alipatikana ameuawa baada ya kupote na kuzua hasira na hofu katika jamii.
Katika tukio lingine la kushtua zaidi, msichana wa miaka 11 aliuawa baada ya kubakwa, kisha mwili wake kuwekwa kwenye mfuko na kuachwa kando ya njia. Polisi wanasema uchunguzi unaendelea, lakini jamii imebaki ikitaka majibu na hatua kali zaidi.
Visa hivi vinaonyesha janga la kitaifa la ukatili dhidi ya wanawake, ambalo limekuwa likihusishwa zaidi na watu wa karibu—wapenzi, waume, na hata wanafamilia. Hali hii imeibua hofu kuwa nyumbani, ambako kunapaswa kuwa mahali salama, kumekuwa hatari kwa wanawake na watoto.
Wataalamu wa masuala ya kijamii wanasema chanzo kikuu ni mchanganyiko wa migogoro ya mapenzi, ukosefu wa mawasiliano, na matatizo ya afya ya akili yasiyotibiwa. Wanasema pia kwamba baadhi ya wahusika hushindwa kudhibiti hasira zao, na hivyo kugeukia ukatili wa hali ya juu.
“Tunashuhudia jamii inayokosa njia za amani za kutatua migogoro,” anasema mtaalamu mmoja wa ushauri nasaha Faith Queen Chebet,, akiongeza kuwa mazungumzo ya mapema yanaweza kuzuia visa vingi vya mauaji.
Wadau wa haki za wanawake wanaitaka serikali kuchukua hatua kali zaidi, ikiwemo kuongeza ulinzi, kuimarisha mifumo ya kuripoti vitisho na kuharakisha mashauri ya mauaji mahakamani. Wanasema kuchelewa kwa haki kunachochea wahalifu kuendelea na ukatili huu.
Hata hivyo, familia nyingi zimebaki zikilia, zikikosa majibu na faraja. Kila kisa kinachotokea kinaacha pengo jipya, na kila kifo kinaongeza presha kwa taifa kuchukua hatua za haraka kabla hali haijazidi kuwa mbaya zaidi.
Kwa sasa, swali kubwa linalobaki mdomoni mwa Wakenya ni moja: nani anaua wanawake hawa, na kwa nini damu yao inaendelea kumwagika bila kukoma?