Maoni

MAONI: Siasa za Magharibi kwa sasa ni mtihani mgumu kwa Ruto

Na PAUL NABISWA May 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

IKIWA kuna mwanasiasa aliyetumia mbinu bunifu kupenya katika siasa za magharibi katika uchaguzi mkuu uliopita alikuwa William Ruto ambaye alikuwa mgombea wa UDA.

Inasemekana kutoka katika pembe tofauti kuwa kaunti ya Bungoma ndiyo iliyomsaidia Ruto kuwa Rais wa tano.

Ili kuonyesha shukrani zake, akamtunuku Moses Wetang’ula kuwa spika wa Bunge la Taifa huku Musalia Mudavadi akifanywa Mkuu wa Mawaziri.

Hata hivyo, eneo hilo linaonekana kuwa na uasi mkubwa kutokana na nguvu changa za Linda Mwananchi ambayo ni merikebu ya Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna.

Pili, Gavana wa Trans Nzoia George Natembeya ana vuguvugu lake la “Tawe” ambalo halitaki kusikia habari za UDA.

Spika Wetang’ula amekuwa na mikutano kuwashawishi wakazi kuunga mkono juhudi za Rais Ruto kupewa muhula wa pili japo kuna upinzani mkubwa.

Katika Kaunti ya Kakamega ambako Rais katika Serikali Jumuishi alimpa kazi Wycliffe Oparanya kuwa waziri wake wa Vyama vya Ushirika na Ustawi wa Biashara ndogondogo, gavana huyo wa zamani wa Kakamega amesema kuwa mzozo katika ODM unawapa yeye na wenzake kazi ngumu mno kumwombea Rais kura.

Kufikia hapo ni kaunti tatu kati ya tano ambapo upinzani umemega kwa kiasi fulani.

Katika kaunti jirani ya Vihiga anakotoka Mudavadi, uwanja wa Rais Ruto ni legevu kwa sababu kadhaa.

Kwanza ODM ilimtimua Seneta Godfrey Osotsi kuwa mmoja wa manaibu viongozi wa ODM.

Osotsi anatoka katika kaunti hiyo na baadhi ya wakazi waliona kuwa alionewa na pia serikali haijawakamata waliomshambulia akiwa Kisumu.

Mkutano wa Linda Mwananchi uliokuwa Vihiga ulidhihirisha kuwa baadhi ya wakazi walikuwa na uchungu na serikali.

Serikali ni UDA na sehemu ya ODM maarufu kama Linda Ground.

Katika mkutano uliofanyika Jumapili iliyopita katika eneo bunge la Bumula na kuongozwa na gavana wa Trans Nzoia George Natembeya, watu walijaaa kama mchanga wa bahari.

Natembeya aliposimama alisisitiza kuwa jamii ya Waluhya itashirikiana licha ya kuwa katika mirengo tofauti ya upinzani yaani ule wa Sifuna wa Linda Mwananchi na ule waliomo Natembeya na washirika wa United Opposition.

Hili la upinzani kusema watakaa pamoja linatakiwa limtie wasiwasi Ruto.

Ikiwa ni kuwatafuta washiriki wengine afanye hivyo kwa dharura kwa sababu inavyoonekana meli za Wetang’ula na Mudavadi inaendelea kuzama katika bahari ya siasa za magharibi.

Hata Busia hali si hali kwa UDA licha ya Gavana Otuoma kuwataka wenyeji wampigie kura Ruto.

  • Paul Nabiswa ni mhariri, NTV