Masuala na dhana msingi katika fani ya ushairi
LEO naomba tuangazie masuala ya kimsingi kuhusu ushairi.
Ushairi ni utungo wa kisanaa unaotumia kanuni/sheria/kaida/arudhi na mpangilio wa lugha ya mkato na yenye mpigo au mdundo maalumu ili kuwasilisha ujumbe uliokusudiwa.
Tuna ushairi huru/mapingiti/mavue/zohari na pia ushairi wa arudhi/ushairi wa kimapokeo.
Sifa za mashairi huru
Huwa hayazingatii idadi sawa ya mishororo katika beti/idadi ya mishororo hutofautiana.
Aghalabu huwa hayana urari wa vina/vina hutofautiana. Huwa hayana idadi sawa ya mizani katika mishororo.
Huwa na kipande kimoja tu.
Hutumia mistari mishata.
Hayana kibwagizo bali huwa na kituo.
Hutumia takriri kwa wingi.
Sifa za mashairi ya arudhi
Huu ni ushairi unaozingatia sheria/kanuni/kaida/kunga katika kuwasilisha ujumbe uliokusudiwa kwa kuzingatia muwala na utoshelevu.
Ili kutambua aina ya shairi, hesabu idadi ya mishororo ili ubaini iwapo bahari ni tathmina, tathnia, tathlitha, tarbia, takhmisa, tasdisa, hasbia, naudia na kadhalika.
Istilahi katika ushairi
Ubeti – ni jumla ya mishororo iliyofungamanishwa pamoja na aghalabu huwa na wazo moja kuu.
Mishororo – ni mistari katika ubeti wa shairi. Mshororo wa kwanza huitwa mwanzo wa pili mloto, wa tatu mleo na wa nne huitwa kibwagizo/mkarara/kiitikio/kipokeo/pambio/wazumi, iwapo mshororo huo unarudiwarudiwa.
Kibwagizo hutumiwa kusisitiza ujumbe, dhamira au nia, kichwa cha ushairi husika na huonyesha mwisho wa ubeti.
Iwapo mshororo wa mwisho unabadilikabadilika, huitwa kituo/kiishio/kimalizio/mwisho na shairi hilo huwa katika bahari ya sabilia.
Vina – ni silabi zenye keketo moja katika mshororo na hupatikana mwisho wa mshororo. Huweza kutiririshwa au vikawa tofauti tofauti.
Vipande – ni mgao wa ubeti. Kipande cha kwanza huitwa ukwapi, cha pili huitwa utao na cha tatu huitwa mwandamizi, cha nne huitwa ukingo.
Mizani – Ni idadi ya silabi au sauti zinazotamkika katika kila mshororo wa ubeti. Mashairi mengi ya arudhi aghalabu huwa na mizani 8, 8, 16. Ingawa si lazima.
Utoshelezi – Ni hali ya shairi kujitosheleza kimaudhui.
Muwala – mtiririko wa mawazo unaosababishwa na kuwepo kwa maudhui kamilifu.
Urari – usawa wa vina au mizani.
Toni/lahani – hisia zinazojitokeza mtu asomapo shairi kama furaha, huzuni, masikitiko, nk. Toni hujikita katika maudhui.
Mistari kifu – mistari inayojitosheleza kimaudhui na kimawazo.
Mishata – mistari/mishororo ambayo haijitoshelezi kimawazo; wazo hukamilikia katika mshororo unaofuata ambao huitwa mstari kifu.
Usambamba – miundo sawa ya sentensi.
Rithimu – mdundo ama mapigo maalum ya mawimbi ya sauti.