Habari

Daktari athibitisha Gachagua alikuwa mgonjwa alipotemwa

Na JOSEPH WANGUI May 14th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

DAKTARI mtaalamu wa moyo Daniel Gikonyo jana aliambia Mahakama Kuu kuwa aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua alikuwa mgonjwa kweli na hakujifanya ili kukwepa Seneti wakati wa mchakato wa kumtimua ofisini huku kicheko, kejeli na majibizano makali yakitawala kikao kilichokuwa na mvutano mkubwa wa kikatiba.

Dkt Gikonyo pia alieleza kuwa alimuarifu Rais William Ruto kuhusu hali ya afya ya Gachagua baada ya kupata idhini yake.

Kikao hicho cha majaji watatu kiligeuka kuwa cha aina ya kipekee, huku mawakili wakipinga stakabadhi za hospitali zinazodai kuwa Gachagua alilazwa Hospitali ya Karen Oktoba 17, 2024 kutokana na maumivu makali ya kifua.

Kiini cha kesi hiyo ni iwapo kulazwa hospitalini kulikuwa kwa kweli au mbinu ya kukwepa kikao cha Seneti kilichoishia kumuondoa madarakani usiku huohuo.

Dkt Gikonyo, mwanzilishi wa Hospitali ya Karen, alisisitiza kuwa mgonjwa alihitaji matibabu ya haraka na alikuwa chini ya uangalizi wake.

“Nilikuwa nikimtibu pamoja na timu yangu. Alikuwa mgonjwa. Tuna data,” alisema.

Mvutano uliongezeka baada ya wakili wa Naibu Rais Prof Kithure Kindiki kudai Gachagua alijilaza hospitalini ili kukwepa Seneti. Kauli hiyo ilisababisha kicheko kortini kabla daktari kupinga.

Alieleza kuwa vipimo vilifanywa na akapendekeza alazwe kwa saa 48 hadi 72 kwa uangalizi.

Majadiliano yalichukua mvutano zaidi kuhusu majina ya mgonjwa, baada ya stakabadhi kuonyesha herufi “R.G” badala ya jina kamili. Daktari alieleza kuwa hilo lilikuwa kulinda faragha ya mgonjwa.

Mahakama iliendelea kujawa na vicheko huku mawakili na daktari wakibadilishana maneno makali kuhusu stakabadhi za matibabu.

Kesi hiyo inaendelea kusikilizwa.