Ufugaji wa viwandani unavyochochea athari za tabianchi
UFUGAJI wa wanyama kwa wingi katika eneo ndogo maarufu kama factory farming, unazidi kulaumiwa kwa kuchangia mabadiliko ya tabianchi, uharibifu wa bioanuwai (biodiversity) na afya ya umma.
Mfumo huu hutumika sana katika ufugaji wa kuku, nguruwe na ng’ombe, ambapo maelfu ya wanyama hufugwa katika mabanda au vizimba vilivyojaa kwa ajili ya uzalishaji wa kibiashara.
Mashirika ya kutetea haki za wanyama na wanaharakati wa mazingira sasa wanataka taasisi za kifedha za kimataifa, zikiwemo Benki ya Dunia, kusitisha ufadhili wa miradi hiyo na badala yake kuelekeza fedha kwa mifumo endelevu inayonufaisha wakulima wadogo.
Kwenye mahojiano ya kipekee na Akilimali Dijitali, Sally Kahiu kutoka World Animal Protection anasema dunia lazima ibadili namna ya kuzalisha chakula.
“Tunashawishi serikali na taasisi kubadili mifumo katili kwa wanyama na kuhamia ile endelevu kwa manufaa ya watu, wanyama na dunia,” alisema. World Animal Protection, ni kati ya mashirika na wanaharakati wanaotetea haki za wanyama zinazoongoza kampeni dhidi ya ufugaji wa viwandani.
Kampeni hiyo imeungwa mkono na zaidi ya mashirika 30 katika nchi 25 kupitia muungano wa Stop Financing Factory Farming. Kulingana na ripoti ya muungano huo, Benki ya Dunia iliwekeza karibu Dola bilioni 1.4 (Sh180.82 bilioni) katika ufugaji wa viwandani kati ya 2023 na 2024 pekee.

Aidha, shirika lake la sekta binafsi, International Finance Corporation (IFC), liliidhinisha uwekezaji 38 wenye thamani ya karibu Dola bilioni 2 (Sh258.34 bilioni) kati ya 2020 na 2025.
Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, pia, limekuwa mpokeaji mkubwa wa fedha hizo, huku likipokea miradi 22 ya mifugo yenye thamani ya Dola bilioni 1.395 (Sh180.19 bilioni), sawa na asilimia 41.9 ya msaada wa moja kwa moja kutoka taasisi za fedha za maendeleo.
Kahiu, ambaye ni Msimamizi wa masuala ya nje Afrika katika Shirika la World Animal Protection, anasema mfumo wa ufugaji wa viwandani una “gharama fiche” kama vile uzalishaji wa gesi chafu, uchafuzi wa maji na hewa, pamoja na ukataji wa misitu kwa ajili ya malisho.
“Chakula cha bei nafuu pekee si suluhisho; tunapaswa kuangalia kinachotutunza kwa muda mrefu,” anaongeza. Ufugaji wa mifugo tayari unachangia pakubwa uzalishaji wa gesi chafu kama methane na nitrous oxide, hasa wanyama wanapokusanywa kwa wingi eneo moja.
Mbali na hilo, mfumo huu unasababisha uharibifu wa ardhi na bioanuwai (biodiversity) kupitia kilimo cha zao moja kwa minajili ya malisho ya mifugo. Ufugaji wa viwandani unachochea matumizi ya antibiotics, dawa ambazo wakulima wanatumia kwa wingi kutibu mifugo.
Wataalamu wanaonya kuhusu matumizi mabaya ya dawa hizi. Dkt Victor Yamo wa Global One Health Advocacy Alliance anasema matumizi hayo huchochea dawa hizo kushindwa kudhibiti maradhi kwa binadamu, ndio, Anti-Microbial Resistance (AMR).

“Hali hii hupunguza ufanisi wa dawa muhimu kwa binadamu na inaweza kusababisha vifo kuongezeka hadi milioni 4.1 barani Afrika kufikia 2050 iwapo hatua za haraka hazitachukuliwa,” anaonya.
Hilo linajiri kupitia ulaji wa nyama, mayai na unywaji wa maziwa, mazao ya mifugo yaliyopewa antibiotics. Mfumo wa factory farming, pia, industrial livestock production, huongeza hatari ya magonjwa yanayotokana na wanyama kusambazwa kwa binadamu (zoonosis) kama vile mafua ya ndege na ya nguruwe.
Hata hivyo, Benki ya Dunia inatetea ufadhili wake. Vera Oloo Rosauer kutoka kwa benki hiyo anasema mifugo ni muhimu kwa lishe, ajira na kipato, na taasisi hiyo ya kifedha inalenga kusaidia uzalishaji endelevu. “Kwa mfano, mpango wa AgriConnect wa World Bank Group unalenga kusaidia wakulima wadogo 500 milioni kuboresha uzalishaji,” Vera anaelezea.
Kwa upande wake Kahiu, anasema Afrika bado ina nafasi kuepuka makosa yanayochochea athari za mabadiliko ya tabianchi. “Tuna mifumo asilia kama vile agroekolojia—kilimo mseto. Kwa nini tusiiwekeze?” anahoji.
Wanaharakati wanasisitiza kuwa mustakabali wa chakula Afrika unategemea uwekezaji kwa wakulima wadogo, utunzaji wa mazingira na mifumo endelevu ya uzalishaji.