Akili Mali

Aina mpya ya muhogo unaostahimili maradhi yanayoharibu zao zima kwa mpigo

Na SAMMY WAWERU May 20th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

JULIA Njagi anatembea kwa umakini katika shamba la majaribio ya ukuzaji wa aina mpya ya mihogo katika Shirika la Utafiti wa Masuala ya Kilimo na Maendeleo ya Mifugo (Kalro), Kandara, Kaunti ya Murang’a.

Anapigia debe aina hiyo ya mihogo, baada ya kushuhudia safari ndefu ya kisayansi iliyochukua zaidi ya mwongo mmoja.

Katika taasisi ya utafiti wa mazao ya bustani ya KALRO, Kandara (HRI), watafiti wamekuwa wakisaka suluhisho dhidi ya magonjwa mawili hatari ya mihogo (cassava brown streak disease na cassava mosaic disease) yanayoweza kuangamiza mazao yote shambani.

Julia, ambaye ni Naibu Mkurugenzi anayesimamia utoaji leseni, ufuatiliaji na usimamizi wa usalama wa viumbe katika Mamlaka ya Kitaifa Kuhusu Usalama wa Bidhaa – National Biosafety Authority (NBA), anasema tangu mwaka 2013, watafiti wamekuwa wakifanyia majaribio mihogo iliyoboreshwa kwa njia ya vinasaba au jeni ili kuhimili magonjwa hayo.

“Magonjwa hayo yanaweza kusababisha hasara ya hadi asilimia 100. Tunachoona hapa ni mihogo inayoweza kujilinda yenyewe,” afisa huyo akaambia Akilimali wakati wa ziara Kalro, Kandara.

Mimea hiyo ya kijani kibichi sasa imekuwa ishara ya matumaini kwa wakulima ambao wamekuwa wakihangaishwa na magonjwa hatari ya mihogo.

Julia Njagi, Naibu Mkurugenzi wa utoaji leseni, ufuatiliaji na usimamizi wa usalama wa viumbe katika National Biosafety Authority (NBA) 2026. PICHA | SAMMY WAWERU

Utafiti uliofanywa Kandara, pamoja na maeneo mengine kama Mtwapa, Alupe, Kakamega na Kiboko tayari umepitia hatua zote za udhibiti zinazohitajika.

Si aina moja ya mihogo pekee. Watafiti wamekuwa wakifanyia majaribio aina kadhaa. Katika shamba la ekari mbili la Kalro Kandara, kwa mfano, kuna aina nane za mihogo iliyoboreshwa.

“NBA imeidhinisha aina hizo baada ya kukamilisha tathmini za usalama na majaribio ya kitaifa ya utendaji,” Julia anadokeza.

Hata hivyo, licha ya mafanikio hayo, mihogo hiyo bado haijafikia wakulima kutokana na kesi zinazoendelea mahakamani kuhusu mazao yaliyoboreshwa vinasaba, au kuimairishwa kisayansi (GMO), nchini Kenya.

Hata hivyo, kulingana na Julia, kazi ya NBA ni kuhakikisha teknolojia zote zilizoidhinishwa ni salama kwa binadamu, wanyama na mazingira.

“Mihogo hii mipya imekidhi viwango vyote vya usalama,” anahakikishia taifa.

Tofauti na pamba ya bt na mahindi ya bt, mazao yake yakilenga kukabiliana na wadudu waharibifu, mihogo iliyoboreshwa inapambana na virusi bila kubadilisha kiwango cha chembechembe za ‘cyanide’ zinazopatikana kiasili.

Wataalamu wa kilimo wanaamini aina hiyo mpya ya muhogo itasaidia kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na kurejesha nafasi ya muhogo kama zao muhimu la kuhakikisha utoshelevu wa chakula.

Kenya tayari imeanza matumizi ya kibiashara ya pamba aina ya Bt tangu mwaka 2020.

Pamba hiyo iliidhinishwa kwa kilimo na biashara mwaka 2019 kufuatia uamuzi wa Baraza la Mawaziri kuondoa marufuku ya mazao yaliyoboreshwa kwa njia ya vinasaba.

Hata hivyo, idhini ya mahindi ya Bt bado imekwama kutokana na kesi zinazoendelea mahakamani kuhusu mazao ya GMO.

Muhogo unaostahimili virusi sasa umejiunga na orodha ya bayoteknolojia na ubunifu unaosubiri kuanza kutumika rasmi, pamoja na maombi mengine ambayo bado yanapitiwa na NBA.

“Uzalishaji wa mbegu unaendelea kwa sasa ili kuhakikisha kuwa pindi vikwazo vya kisheria vitakapoondolewa, wakulima watapata mbegu za kutosha za kupanda,” Julia anasema.

Majaribio ya aina hiyo mpya ya muhogo yanatekelezwa kupitia mradi wa Virus Resistant Cassava for Africa (ViRCA) Plus kwa ushirikiano na KALRO, na Beatrice Wambui ni mmoja wa wahudumu.

Anasema, katika uzalishaji, kiwango chake ni cha hali ya juu.

“Mmea mmoja unaweza kutoa kilo nne hadi tano, na hukomaa kwa haraka zaidi, karibu miaka miwili, ikilinganishwa na zaidi ya miaka miwili na nusu kwa aina za kitambo,” anasema.

Aidha, Beatrice amekuwa akifanya kazi na mradi huo tangu 2015.

Mbali na mavuno mengi, aina hiyo mpya ya muhogo ina uwezo mkubwa kustahimili magonjwa na athari za tabianchi.

Kaunti za Busia, Kilifi, Migori na Homa Bay zinaongoza kwa uzalishaji wa muhogo nchini Kenya, huku watafiti wakiamini teknolojia hiyo mpya inaweza kuongeza uzalishaji na kurejesha matumaini kwa wakulima wa mashamba madogo.