Chama chaitisha maandamano kupinga kupanda kwa bei ya mafuta nchini
CHAMA cha wenye magari nchini Kenya (MAK) kimetoa ilani ya mgomo wa kitaifa, kikionya kuwa shughuli zitakwama nchi nzima kuanzia Jumatatu kulalamikia ongezeko la hivi majuzi la bei za mafuta.
Chama hicho, pamoja na wadau mbalimbali wa sekta ya usafiri, kimesema mgomo huo utaathiri sekta muhimu ikiwemo usafiri wa umma, usafirishaji wa mizigo, vifaa na madereva binafsi kote nchini.
Katika taarifa iliyotolewa kupitia mitandao ya kijamii Ijumaa, kufuatia mkutano wa ngazi ya juu wa wadau uliofanyika Nairobi, chama hicho kimesema uamuzi huo ulifikiwa kwa kauli moja kutokana na kile kilichotaja kama “ongezeko lisilo na msingi la bei za mafuta” lililotangazwa na Mamlaka ya Kudhibiti Kawi na Petroli (EPRA).
Wadau wanadai marekebisho ya bei ya mafuta yaliyofanyika Mei 14 yameongeza gharama ya maisha, na kusababisha kupanda kwa nauli na bei ya bidhaa za msingi.
“Chini ya mwavuli wa Muungano wa Uchukuzi, vyama vya sekta ya usafiri vinatoa ilani ya mgomo wa kitaifa kuanzia Jumatatu, Mei 18, 2026, kulalamikia ongezeko endelevu na lisilo na msingi la bei za mafuta lililowekwa na Serikali kupitia EPRA,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
“Kufuatia mkutano wa pamoja wa wadau wa ngazi ya juu uliofanyika leo( Ijumaa) Nairobi, wawakilishi kutoka sekta mbalimbali walikubaliana kwa kauli moja kuanza mgomo wa kitaifa na maandamano ya amani.”
Mgomo huo unatarajiwa kuhusisha makundi mbalimbali yanayotegemea mafuta, wakiwemo wamiliki na wahudumu wa matatu, bodaboda, madereva wa teksi, wasafirishaji wa mizigo na bidhaa, wahudumu wa magari ya utalii, madereva binafsi, pamoja na wachimbaji wa visima na jenereta.
Muungano huo umetoka matakwa kadhaa ikiwemo kufutwa mara moja kwa ongezeko la hivi karibuni la bei za mafuta, kusawazishwa upya kwa mfumo wa bei ya mafuta ili kuzuia kuvurugwa kwa soko, kuvunjwa kwa EPRA ambayo wanailaumu kwa kuruhusu gharama za juu za mafuta, na kuruhusu ushindani katika bei za mafuta.
Pia wamelaumu serikali kwa kuchangia mfumuko wa bei kupitia sera wanazoita ushuru wa mafuta wa kukandamiza.
Chama hicho kimewataka Wakenya wote walioathiriwa kuunga mkono maandamano hayo, kikionya kuwa nchi inaweza kukumbwa na usumbufu mkubwa wa usafiri iwapo malalamiko yao hayatashughulikiwa.
“Muungano wa Uchukuzi unawataka Wakenya wote wanaoathirika na mzigo wa bei kubwa ya mafuta na kupanda kwa bei ya bidhaa kujiunga na maandamano ya kitaifa kuanzia Jumatatu. Hii ni hatua ya pamoja ya kutafuta haki ya kiuchumi, usawa na kulinda maisha ya wananchi,” ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Awali, MAK ilikuwa imeeleza wasiwasi kuhusu marekebisho ya bei ya mafuta, ikihoji mantiki ya ongezeko la petroli na dizeli huku bei ya mafuta ya taa ikikosa kubadilika.
Katika taarifa ya Ijumaa, chama hicho kilisema hali hiyo inaonyesha ukosefu wa uwazi katika maamuzi ya serikali.