Watu 4 watoweka baharini upepo mkali ukivuma Pwani
WATU wanne wameripotiwa kupotea huku wengine wanne wakiokolewa baada ya boti kuzama Lamu.
Meneja wa Kituo cha Dharura cha Kaunti ya Lamu (EOC) Iftakhar Majid, alithibitisha tukio hilo, akisema boti kwa jina la ‘Buraq’ ilikumbwa na upepo mkali pamoja na mawimbi na hatimaye kuzama katika eneo la Sinda Kasi karibu na mkondo wa Manda-Bruno.
Boti hiyo iliyokuwa imebeba mzigo wa nguzo za mikoko na mbao pamoja na watu wanane ilikuwa ikitoka Kiangwe katika Msitu wa Boni, Kaunti Ndogo ya Lamu Mashariki kuelekea Kisiwa cha Lamu kilicho Lamu Magharibi.
Boti hiyo ilipinduka mwendo wa saa tatu usiku wa Jumatano.
Manda-Bruno ni mojawapo ya njia za majini zinazojulikana kuwa hatari na zenye mawimbi makali katika maji ya Bahari ya Hindi eneo la Lamu.
“Taarifa hizo zilitoka kwa mmoja wa manusura ambaye aliponea baada ya kusombwa hadi ufukweni na baadaye kuokolewa na kikosi cha doria cha Kitengo cha Usimamizi wa Ufukwe (BMU),” alisema Bw Majid.
Aliongeza kuwa, taarifa za dharura zilifikishwa kwanza kwa Huduma ya Walinzi wa Pwani nchini (Kenya Coast Guard Service) mwendo wa saa tano asubuhi Alhamisi.
Bw Majid alisema shughuli za uokoaji zilianzishwa mara moja baada ya taarifa hizo kupokewa.
Kufikia Alhamisi alasiri, operesheni ya pamoja ya utafutaji na uokoaji ilikuwa imeimarishwa lakini watu wote wanne waliokuwa wamepotea walikuwa bado hawajapatikana.
“Tunawaomba watumiaji wote wa bahari na wananchi ambao wana taarifa zozote kuhusu tukio hili au watu waliopotea kuwasiliana nasi haraka kupitia nambari yetu ya dharura 0714-888-889,” alisema.
Aliwataka familia na marafiki wa walioathirika kuwa na subira na kushirikiana katika kipindi hiki kigumu huku timu za uokoaji zikiendelea na operesheni.
Kulingana na Mamlaka ya Huduma za Hali ya Hewa nchini, upepo mkali unatarajiwa kuathiri eneo la Pwani wiki hii pamoja na sehemu za Mashariki na Kaskazini Mashariki mwa Kenya.
Kwa mujibu wa idara hiyo, upepo huo mkali ulitabiriwa kushuhudiwa katika eneo la Pwani na Kaunti za Turkana, Marsabit, Garissa, Mandera, Wajir, Isiolo, Makueni na Kitui.
Upepo huo unaovuma kutoka kusini na kusini mashariki unatarajiwa kuzidi kasi ya zaidi ya kilomita 46 kwa saa.
Hali hiyo inaweza kusababisha mawimbi makubwa na kuvuruga shughuli za baharini, mbali na kusababisha uharibifu kwa miundombinu dhaifu na kuangusha miti.
Mchanganyiko wa upepo mkali na mawimbi makubwa huwa hatari kwa vyombo vidogo vya majini kwa kuwa husababisha bahari kuwa na mawimbi makali na kupunguza uwezo wa kuona.
Mamlaka zimekuwa zikiwataka waendeshaji wa shughuli za baharini kutilia maanani tahadhari zinazotolewa na kuepuka maeneo ya kina kirefu na bahari ya wazi kila wakati Bahari ya Hindi inaposhuhudia upepo mkali na mawimbi makubwa.
Ajali hiyo imejiri takriban wiki mbili baada ya mwanamke na mtoto wake wa miezi tisa kufariki dunia baada ya boti mbili kugongana katika Mkondo wa Kilindini, Lamu, kwenye Bahari ya Hindi.
Watu wengine 14 waliokuwa ndani ya vyombo hivyo viwili pia walijeruhiwa huku wawili kati yao wakipata majeraha mabaya.