Habari za Kitaifa

Arsenal watawazwa mabingwa wa EPL kwa alama 85

Na MASHIRIKA May 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

LONDON, Uingereza:

ARSENAL hatimaye walitawazwa mabingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) kwa jumla ya alama 85 Jumapili baada ya kushinda mechi yao ya mwisho ugenini dhidi ya Crystal Palace.

Mechi hiyo haikuwa na maana yoyote kwa sababu tayari timu hiyo ya London Kaskazini ilikuwa imetwaa taji hilo baada ya kufungua mwanya wa alama nne baina yake na Manchester City iliyokuwa inafuatia.

Mabao ya Gabriel Jesus katika dakika ya 41 na Noni Madueke (47) yalitosha kuipa Arsenal alama tatu baada ya kuwalemea wenyeji wake kwa magoli 2-1.

Jean-Philippe Mateta aliwakombolea Palace bao moja katika dakika ya 88.

Kwingineko, bao la Joao Palhinha katika dakika ya 43 dhidi ya Everton, lilitosha kuinusuru Tottenham Hotspur dhidi ya mkosi wa kushuka daraja katika mechi ya mwisho ya EPL Jumapili.

West Ham United ambao pia walikuwa wakipigania kusalia ligi kuu, walihitaji Spurs kupoteza nao washinde ili kujinasua kutoka kwa shoka hilo.

Lakini hata baada ya West Ham kutimiza wajibu wao kwa kuichapa Leeds United 3-0, walishushwa ngazi.

Valentín Castellanos alicheka na wavu wa kwanza dakika ya 67 kabla ya Jarrod Bowen kuongeza la pili dakika ya 79 ya mchezo kabla ya Callum Wilson kufunga ukurasa wa mabao na bao la tatu dakika za lala salama kipindi cha pili, Spurs walimaliza msimu katika nafasi ya 17 kwa alama 41, mbili zaidi ya West Ham, huku pia wakijivunia pengo la mabao 12 dhidi ya West Ham.

Sasa West Ham chini ya Nuno Espírito Santo watacheza ligi ya daraja ya pili, Championship msimu ujao.

West Ham sasa watajiunga na Wolves na Burnley ambao tayari walikuwa wameaga mapema ligi kuu kuelekea Championship.

Nao Manchester City ambao walipokea kichapo cha mabao 2-1 dhidi ya Aston Villa walimaliza wa pili kwa alama 78.

Machester United ya kocha Michael Carrick walifunga tatu bora kwa alama 71 baada ya kuinyorosha Brighton 3-0 ugani American Express.

Sasa Arsenal, Manchester City, Manchester United, Villa na Liverpool ambao walitoka sare ya 1-1 wamemaliza katika nafasi tano-bora kwenye jedwali na kufuzu kwa kipute cha Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) msimu ujao.

AFC Bournemouth baada ya kutoka sare ya 1-1 na Nottigham Forest na Sunderland ambao waliwapepeta Chelsea 2-1 watashiriki UEFA Uropa League msimu ujao, baada ya kumaliza katika nafasi ya sita na saba mtawalia.

Brighton nao walimaliza nafasi wa nane hivyo basi kufuzu kushiriki michuano ya kufuzu UEFA Conference League.

Matokeo:

Brighton 0-3 Man United, Burnley 1-1 Wolves, Crystal Palace 1-2 Arsenal, Fulham 2-0 Newcastle, Liverpool 1-1 Brentford, Manchester City 1-2 Aston Villa, Nottm Forest 1-1 Bournemouth, Spurs 1-0 Everton, Sunderland 2-1 Chelsea, West Ham 3-0 Leeds.