Habari

Mabinti waliozaliwa nje ya ndoa washinda kesi ya urithi

Na BENSON MATHEKA May 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAHAKAMA Kuu imebatilisha uamuzi wa mahakama ya chini uliokuwa umempa mjane theluthi mbili ya mali ya marehemu mumewe, ikisema watoto waliozaliwa nje ya ndoa wana haki ya kurithi mali.

Kilichoanza kama mzozo wa kawaida wa urithi kuhusu mamilioni ya pesa yaliyokuwa katika akaunti ya benki, kiligeuka kuwa vita vya kisheria.

Kiini cha mzozo huo alikuwa mwanaume aliyefariki akiacha nyuma mke aliyekuwa ametengana naye, watoto watatu ndani ya ndoa na mabinti wawili waliozaliwa nje ya ndoa.

Kwa miezi kadhaa familia hiyo ilivutana mahakamani kuhusu nani angeongoza usimamizi wa mali ya marehemu na namna mali hiyo ingegawanywa.

Hatimaye kesi hiyo ilifika Mahakama Kuu ya Kajiado, ambapo uamuzi wa mahakama haukubadilisha tu ugavi wa mali bali pia ulituma ujumbe kuhusu haki katika migogoro ya urithi inayohusisha familia ambazo hazina muundo.

Jaji alibatilisha uamuzi wa awali uliokuwa umempa mjane nguvu kubwa katika usimamizi wa mali huku watoto wengine wa marehemu wakipata sehemu ndogo zaidi.

Mwisho wa kesi hiyo, mahakama ilirejesha haki za mabinti waliozaliwa nje ya ndoa, ikimteua mmoja wao kuwa msimamizi mwenza wa mali hiyo na kusisitiza kuwa haki na usawa vinafaa kuongoza migogoro ya urithi badala ya kutegemea tu masharti ya kiufundi ya sheria.

Kesi hiyo iliwasilishwa na Lucy Gathoni Njama aliyedai kuwa mjane halali wa marehemu.

Kulingana na rekodi za mahakama, aliwasilisha ombi la kusimamia mali hiyo na baadaye kupendekeza mfumo wa ugavi uliokuwa ukimpendelea zaidi.

Hatua hiyo ilipingwa na mabinti wawili wa marehemu waliodai kuwa ingawa mama yao hawakuolewa na marehemu, wao ni watoto wake wa damu na hivyo wana haki sawa ya kurithi.

Mahakama ilisema kutengana kwa wanandoa hakuvunji ndoa chini ya Sheria ya Urithi.

Hata hivyo, jaji alisisitiza kuwa haki za watoto wote lazima zilindwe.

Mahakama pia ilitupilia mbali mfumo wa ugavi uliokuwa umempa mjane theluthi mbili ya mali huku watoto watano wakigawana theluthi moja pekee, ikisema ulikuwa wa ubaguzi mkubwa.

Katika uamuzi mpya, mjane alipata asilimia 40 ya mali huku kila mtoto akipata asilimia 12.

Zaidi ya hoja za kisheria, kesi hiyo imeonyesha jinsi familia za kisasa nchini zinazokumbwa na migogoro kuhusu urithi.