Habari za Kitaifa

Mkataba wa mauti? Maswali Kenya ikiruhusu Amerika kuleta wagonjwa wake wa Ebola humu nchini

Na ANGELA OKETCH, MERCY CHELANGAT May 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

SERIKALI ya Amerika inapanga kuwaleta Kenya raia wake wanaoambukizwa na virusi vya Ebola, hatua ambayo imeibua maswali makubwa kuhusu uwazi, usalama wa afya ya umma na misingi ya kisheria ya makubaliano hayo.

Ingawa serikali ya Kenya inakiri kuwa kuna mazungumzo yanayoendelea, imekataa kutoa maelezo ya msingi kuhusu mpango huo, na hivyo kuacha pengo kubwa la taarifa kwa umma.

Wakati Taifa Leo ilipotuma maswali kwa Waziri wa Afya Aden Duale kuhusu iwapo Kenya imeruhusu Amerika kuwa na kituo cha kutenga wagonjwa wa Ebola nchini, kitakapojengwa na lini kitaanza kazi, wizara haikujibu moja kwa moja swali lolote kati ya hayo.

Badala yake, Bw Duale alitoa taarifa ya kurasa mbili ikithibitisha kuwa Kenya iko katika “mazungumzo yanayoendelea” na serikali ya Amerika pamoja na washirika wa kimataifa kuhusu maandalizi ya Ebola.

Alisema Kenya “inakubali ushirikiano unaoimarisha usalama wa afya duniani” na iko “tayari na ina uwezo,” lakini hakuthibitisha kuwepo au kuidhinishwa kwa kituo cha kuwatenga wagonjwa.

Taarifa hiyo haikueleza ni nani aliidhinisha mpango huo, umeegemea sheria gani, au athari zake kwa usalama wa Wakenya.

Vyombo vya habari vya kimataifa, ikiwemo The Wall Street Journal, The New York Times na Reuters, viliripoti kuwa utawala wa Trump unapanga kutuma maafisa wa afya wa Amerika nchini Kenya ili kusimamia kituo kitakachotumika kuwatenga raia wa Amerika wanaoshukiwa au kuambukizwa Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Uganda.

Baadhi ya wanachama wa Huduma ya Afya ya Umma ya Amerika tayari wameripotiwa kupokea notisi za kutumwa kazini Kenya.

Kwa mujibu wa Reuters, Kituo cha Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa cha Amerika (CDC) pia kimeomba wafanyakazi kujitolea kusaidia uchunguzi wa Ebola katika vituo vya kuingia Kenya.

Kufikia Jumanne, kituo hicho hakikuwa kimepata idhini ya mwisho ya serikali ya Kenya.

Taifa Leo iliwasilisha maswali kumi kwa Waziri Duale kuhusu msingi wa kisheria wa mpango huo, eneo la kituo hicho, muda wa utekelezaji, na hatua za usalama wa afya.

Hakukuwa na majibu ya moja kwa moja kuhusu iwapo Amerika iliwasilisha ombi rasmi, nani aliidhinisha, au ni chini ya sheria gani mpango huo utatekelezwa.

Pia, hakujibu iwapo kituo hicho kiko chini ya mfumo wa ushirikiano wa afya uliopo kati ya Kenya na Amerika, au kama ni mpango mpya unaojitegemea.

Kenya, kwa sasa ina uwezo mdogo wa kushughulikia Ebola, ikiwa na kituo kimoja cha kuwatenga wagonjwa katika Hospitali ya Kitaifa ya Kenyatta na maabara chache zinazoweza kuthibitisha virusi hivyo.

Nchi hii pia haina chanjo au tiba iliyoidhinishwa kwa aina ya Ebola inayofahamika kama Bundibugyo inayosambaa katika baadhi ya maeneo ya Afrika Mashariki.

Katika mazingira haya, mpango wa Amerika wa kuleta raia wake wanaoambukizwa virusi hivyo na kuwatenga nchini Kenya umeibua maswali zaidi kuliko majibu.

Hata hivyo, baadhi ya maafisa wa serikali wanasema mpango huo ni sehemu ya maandalizi mapana ya kikanda yanayohusisha Kenya, Amerika na washirika wengine wa kimataifa, ikiwemo Uingereza.

Wanasema Kenya imechaguliwa kutokana na nafasi yake ya kijiografia, miundombinu ya usafiri wa anga, na mchango wake katika usalama wa afya ya kikanda.

Wataalamu wa magonjwa ya kuambukiza wametoa maoni tofauti kuhusu mpango huo.

Baadhi yao wanasema kituo cha kuwatenga wagonjwa nchini Kenya kinaweza kusaidia kupunguza hatari ya maambukizi kimataifa kwa kuwazuia watu walio na virusi hivyo kusafiri umbali mrefu wakati wa kipindi cha siku 21 cha kupevuka kwa Ebola.

Wanasema hatua hiyo inaweza kupunguza hatari katika safari za ndege za kimataifa na kusaidia kufuatilia watu waliowekwa chini ya uangalizi wa matabibu.

Hata hivyo, wataalamu wengine wanaonya kuwa kituo kama hicho kinahitaji mifumo madhubuti ya usalama wa maabara, uangalizi wa kitaifa na kimataifa, pamoja na uwazi kamili wa kisheria.

Wanasema bila udhibiti wa Kenya, mpango huo unaweza kuibua hatari za usalama na changamoto za uwajibikaji wa afya ya umma.

Maafisa wanaoshiriki mazungumzo hayo wanasema kituo hicho bado hakijakamilika wala kuanza kazi.

Wanasema huenda kikawa cha muda kwa ajili ya kuwatenga na kufuatilia wagonjwa kabla ya kuhamishwa, badala ya kuwa kituo cha matibabu kamili.