KINAYA: Sifurahii kwamba RAO amefufukia Senegal!
KWANI RAO amefufukia Afrika Magharibi? Nchini Senegal kuna mwanasiasa ambaye ana tabia za RAO, na nimeanza kuwaonea wivu.
Roho ya RAO inapaswa kusalia Kenya ili tuitumie kuchokoza viongozi wetu.
Natamani mtu wa kuisumbua serikali! Laiti RAO angalikuwa hai, aisumbue ilimradi tu. Serikali haipaswi kuruhusiwa kuwa na amani.
Itatudhani wajinga au wavivu, ianze kufanya ya hovyo.
Kizazi kichanga cha Gen-Z kinafanya kazi nzuri ya kuihangaisha serikali, lakini tunahitaji nguvu zaidi ili tutungiwe sheria bora kupitia miswada bungeni.
Wala usiniambie RAO alipenda pesa sana, eti alipokezana mikono ya maridhiano na viongozi kadha wa nchi yetu, labda akakabidhiwa kitita fulani cha hela.
Huyo ni RAO mzee; mchanga alikuwa moto wa kuotea mbali. Msumbufu kama nini!
Nchini Senegal ametokea mwanasiasa kwa jina Ousmane Sonko, akawakosesha usingizi viongozi wote. Sonko alikuwa waziri mkuu hadi kufikia wiki jana, lakini akafutwa kazi ghafla na Rais Bassirou Diomaye Faye.
Siku chache baadaye, bunge la nchi hiyo lilimchagua Sonko spika, jambo ambalo limemshtua sana Rais Faye!
Kisa na maana? Sonko anaweza kuwashawishi wabunge wamfute kazi Rais Faye! Mwindaji amekuwa mwindwa hata kabla hatujapepesa macho!
Sonko hajaanza janja zake jana. Kutokana na umaarufu na usumbufu wake, alisingiziwa mashtaka ya ubakaji, kesi ikaendelea kwa muda mrefu hivi kwamba hangewania urais katika uchaguzi uliopita.
Ili kuonyesha kwamba ndiye bosi wa kweli, alitangaza kumuunga mkono mwaniaji wa urais wakati huo, Bw Faye, akashinda kwa urahisi, ndiposa akamteua Sonko waziri mkuu.
Na kwa sababu hulka ya Sonko ni ya mja asiyewahi kutulia, wawili hao walianza kusumbuana. Rais Faye aliamua kuuma mkono uliomlisha, Sonko. Mkono wenyewe umekataa kukatika, na ndiyo maana sasa unaitwa spika, na unatishia kumnyonga Faye mwenyewe.
Kila mtu anajua hivyo, na tunafurahia si haba. Kwa nini? Binafsi simpendi msaliti. Rais Faye alidhani keshafika alikotaka kwenda, hamhitaji Sonko tena. Basi na yamkute ya kumkuta. Aliyataka mwenyewe.
Hiyo ndiyo tabia ya mwanasiasa mkora; anakutumia kama ngazi kukwea hadi kwenye paa, kisha anakupiga teke na kukuangusha ili usimfikie, au utumiwe na mwingine kumfikia. Sasa Sonko anatishia kubomoa nyumba nzima na Rais Faye hana kwa kujificha.
Ukenya wangu unaniambia kuwa vituko vya aina hiyo havifai kufanyika kwingine duniani ila Kenya. Dunia inatujua kwa vituko na sarakasi za kisiasa.
Sasa ona, Wasenegali wanapata umaarufu wote huo, nasi tumegeuka mashabiki wa kawaida tu.
Hebu na tuchangamke, tuige tabia za RAO, tuishinikize serikali kututawala vizuri, umaarufu urejee kwetu, asije akathubutu mtu kutukandamiza.
– Douglas Mutua ni mwanahabari Mkenya anayeishi Amerika ([email protected])