Lenku, mdhibiti wa Ikulu wavutania kesi ya mwanahabari
GAVANA wa Kajiado, Joseph Ole Lenku na Mdhibiti wa Ikulu Katoo Ole Metito wanavutana kuhusu fidia ya Sh16 milioni.
Viongozi hao wawili wa kisiasa wametofautiana vikali kuhusu kesi ambayo Bw Metito aliwasilisha dhidi ya Jonathan Teikan, mhariri wa Kajiado Star, tovuti ya habari mtandaoni, kutokana na taarifa kuhusu ardhi ambayo mwanahabari huyo alichapisha.
Kiini cha mvutano huo ni harambee inayotarajiwa kufanyika Ijumaa katika Uwanja wa Ildamat kwa lengo la kumsaidia Teikan kulipa fidia hiyo.
Harambee hiyo itaongozwa na Gavana Lenku kama mgeni mkuu baada ya familia ya mwanahabari huyo kumuomba msaada.
Seneta wa Kajiado Samuel Seki pamoja na wabunge kadhaa wakiongozwa na Mbunge wa Kajiado Kusini, Samuel Parashina na Seneta Peris Tobiko wametangaza kuwa watahudhuria hafla hiyo ya kuchangisha fedha.
Kajiado Star ni tovuti ya habari inayoripoti masuala ya jamii ya Maa na yenye makao yake mjini Kajiado.
Bw Metito amekosolewa kwa kukataa juhudi za maridhiano zilizofanywa na familia ya Teikan.
Badala yake, amedai familia hiyo imekuwa ikituma wajumbe kumshawishi aondoe kesi hiyo.
Akiwa mahakamani, Bw Metito alisema makala iliyochapishwa iilimpaka tope kama kiongozi wa muda mrefu serikalini na katika jamii.
Amesisitiza kuwa hatua yake ya kwenda kortini ilikuwa ya kulinda jina lake dhidi ya taarifa za kumpaka tope.
Mnamo mwaka 2024, Bw Metito alimshtaki Teikan kwa kuchapisha habari iliyomhusisha na unyakuzi usio halali wa ardhi katika Rombo Group Ranch, Kajiado Kusini.
Mnamo Oktoba 24, 2025, Mahakama ya Ngong iliamua kuwa Teikan amlipe Bw Metito Sh16 milioni, zikiwemo Sh15 milioni za fidia na Sh1 milioni kwa kumharibia jina, mateso ya kihisia na kuathiri hadhi yake kitaaluma.
Mahakama pia ilitoa amri ya kudumu ikimzuia Teikan kumhusisha Bw Metito na shughuli zozote za ardhi zinazohusu Rombo Ranch.
Harambee hiyo sasa imezua mgawanyiko mkubwa wa kisiasa huku wafuasi wa gavana Lenku wakisaka michango na wale wa Bw Metito wakisema suala hilo limegeuzwa uhasama wa kisiasa.Babake Teikan, Jackson Kutatoi, alisema familia ilikuwa imefikia hatua ya kutaka kuuza ardhi ya familia ili kulipa fidia hiyo kabla viongozi wa eneo hilo kuingilia kati na kupendekeza harambee ya jamii.
“Sh16 milioni ni fedha nyingi sana kwa familia inayohangaika kama yetu. Tunaomba watu wenye nia njema wajitokeze kutuunga mkono,” alisema Kutatoi.
Alisema juhudi za kutatua mzozo huo kwa njia ya kitamaduni zilikwama baada ya Bw Metito kukataa maombi yao yaliyowasilishwa kupitia viongozi waliochaguliwa.
Wakati huo huo, wanahabari wengine wawili wanatarajiwa kufikishwa katika Mahakama ya Ngong kujibu kesi nyingine za madai ya kumpaka tope Bw Metito zilizochapishwa kwenye mitandao ya kijamii.